Uwepo wa Site hii Unategemea sana Ushirikiano wangu na wako, na ni njia mojawapo ya kuonyesha mshikamano na Jamii inayotuzunguka , PLS Usisite kunitumia Habari au kitu chochote chenye Uhakika ambacho hisia zako zitakupeleka kuwa kitaleta Mabadiliko na mafunzo katika jamii, Kumbuka kuwa msaada si Fedha wala Lulu bali chochote kinachoweza kuleta mabadiliko katika Maisha ya mtu mwingine. Kwa lolote usisite kuwasiliana nami kupitia chingasite@gmail.com au tumainijhn@yahoo.co.uk au simu No. 0712221744 na 0787221744. Karibuni Wote
Powered By Blogger

Thursday, December 31, 2009

Pigo kubwa Tanzania - Simba wa Vita afariki Dunia Leo

WAZIRI Mkuu wa za zamani, Mzee Rashidi Mfaume Kawawa 'Simba wa vita' amefariki dunia leo asubuhi. Mzee Kawawa alikuwa ni Waziri Mkuu wa kwanza wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania wa Awamu ya Kwanza ya Baba wa Taifa, MWalimu Julius Kambarage Nyerere. Kawawa amefariki dunia leo asubuhi,31,Desember, 2009, akiwa na umri wa miaka 83. Rais Jakaya Kikwete ametangaza siku saba za maombelezo ya kitaifa ya kifo cha Mzee Kawawa na kwa wakati huo bendera za taifa zitapepea nusu mlingoti. Mungu ailaze roho ya marehemu mahali pema peponi
Amina

Amuua Mkewe kwa kujifungua mtoto wa Kike!!!!!!!!!!!!!

Daniel Hicks mwenye umri wa miaka 29 mkazi wa Seattle (pichani katikati), Washington nchini Marekani anatafutwa na polisi baada ya kumuua mkewe na mtoto wake mchanga wa kike mwenye umri wa miezi mitatu(pichani). Daniel alifanya mauaji hayo kwa kuwa alikuwa hajaridhia mkewe Jenifer Morgan mwenye umri wa miaka 28 kujifungua mtoto wake. Daniel alimwonya mkewe wakati wa ujauzito wake kuwa iwapo atajifungua mtoto wa kike basi atamkataa yeye na mtoto atakayejifungua. Miezi mitatu baada ya mkewe kujifungua mtoto wa kike, Daniel alishindwa kuzizuia hasira zake na kumuua mkewe pamoja na mtoto wake mchanga kabla ya kutoroka na kujificha sehemu isiyojulikana. Daniel alimuua mkewe kwa kumpiga risasi 12 na hakuwa na huruma hata kidogo kwa mtoto wake mchanga ambaye alimuua kwa kumtandika risasi 7. Daniel kabla ya kutoroka aliacha ujumbe akisema kuwa anasikitika yeye pia ana ugonjwa kama wa babu yake.Mnamo mwaka 1983 , Babu yake Daniel alimuua mkewe kwa kumpiga risasi kabla ya kujimaliza mwenyewe.

Mwanamke Asakwa Dar kwa Mauaji ya kichanga

Mama mmoja Jijini Dar anasakwa na Jeshi la Polisi baada ya kukisokomeza kichanga chake kwenye mfuko wa rambo na hatimaye kukisababishia kifo. Kamanda wa Mkoa wa Kipolisi Temeke, Liberatus Sabas, amesema mama huyo aliweza kutekeleza unyama wa kumtumbukiza mwanae ndani ya mfuko wa rambo na kisha akaenda kumtupa na hatimaye kumsababishia kifo, ikiwa ni muda mfupi tu baada ya kujifungua.  kichanga hicho kiligundulika majira ya saa 3:30 usiku na wakazi wa eneo hilo la Temeke, kabla ya kufanya utaratibu wa kuripoti tukio hilo polisi. Hata hivyo, akasema polisi walipofika eneo hilo la tukio, walikuta kichanga hicho tayari kimefariki na mwili wake wakaupeleka katika Hospitali ya Wilaya ya Temeke. Kamanda Sabas akasema juhudi za kumtafuta mwanamke huyo zinaendelea ili akipatikana aweze kufunguliwa kesi ya kuua.

Mashoga wa Kwanza kufunga ndoa Nchini Argentina


Alex Freyre mwenye umri wa miaka 39 na Jose Maria Di Bello mwenye umri wa miaka 41 (pichani) wamekuwa watu wa kwanza kufunga ndoa za jinsia moja katika nchi za Latin America.
Alex alifunga ndoa na mpenzi wake Jose katika harusi iliyofanyika katika mji wa Ushuaia kusini mwa Argentina .Mashoga hao ambao wote wana ugonjwa wa ukimwi awali walipanga kufunga ndoa yao desemba 1 ambayo ni siku ya ukimwi duniani lakini jaji wa mahakama moja nchini humo aliweka pingamizi la kufanyika kwa ndoa hiyo. Jose na Alex walipata kibali cha kufunga ndoa ya jinsia moja mwezi novemba mwaka huu na kupewa ruhusa na mahakama kufunga ndoa katika mji mkuu wa nchi hiyo Buenos Aries.

Mchungaji huyu Adaiwa Kutekwa


Mchungaji huyo wa kanisa la kijiji cha Makurunge, inadaiwa alitekwa juzi. Kaka wa mchungaji huyo, Bw. Emmanuel Ntungu ameyaambia baadhi ya magazeti kuwa tangu jana usiku yuko na askari polisi wakijaribu kumtafuta ndugu yake ambaye inadaiwa amefichwa na watekaji kwenye jumba moja lililo karibu na bahari. “Jana niliitwa polisi wakanihoji na jioni waliandika maelezo…ndipo kazi ya kuanza kumsaka ikaanza lakini hadi sasa hatujaambulia kitu,’’ amesema.Amesema ndugu zao wengine wameanza kuzunguka kwenye hospitali mbalimbali na vituo vya usalama kujaribu kumtafuta Mchungaji Michael. Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kipolisi wa Kinondoni Mark Kalunguyeye, amesema bado wanafuatilia tukio hilo.

Ataka kuua baada ya kunyimwa Penzi kinyume na Maumbile

OMARI Mohamed (22), mkazi wa Yombo jijini Dar es Salaam, amefikishwa katika Mahakama ya Wilaya ya Temeke kujibu, shtaka la kutaka kumuua msichana baada ya kukataa kumwingilia kinyume na maumbile. Akisoma hati ya mashitaka, Inspekta Isaya Mwanga mbele ya Hakimu Aziza Kalili wa mahakama hiyo alidai kuwa,mshitakiwa alitenda kosa hilo Oktoba 10, mwaka huu katika majira ya saaa 2 usiku huko Yombo Kilakala. Alidai baada ya mshitakiwa kumwambia mlalamikaji kuwa alikuwa anahitaji kumwingilia kinyume na maumbile mlalamikaji alikataa kufanyiwa kitendo hicho na ndipo Omari alimchoma kisu cha tumbo, mgongoni na kwenye ubavu jambo ambalo lilimsababishia kuzirai na kupoteza fahamu papohapo. Alidai hali hiyo ilimfanya mlalamikaji apoteze fahamu papohapo na kukimbizwana wasamaria wema katika hospitali ya Taifa Muhimbili kwa matibabu zaidi. Mlalamikaji baada ya siku mbili aliweza kupata fahamuna kueleza umma jinsi ilivyokuwa na mshitakiwa kwenda kukamatwa Hata hivyo mshtakiwa alipotakiwa kujibu shtaka hilo, alikana na alipelekwa rumande kwa kukosa dhamana, na kesi imeahirishwa hadi Januari 7, mwaka huu itakapotajwa tena.

Monday, December 21, 2009

Mahabusu watoroka chini ya Ulinzi wa POLISI!!!!!!!!!!!!

Mahabusu watatu wanadaiwa kutoroka chini ya ulinzi wa askari wa Jeshi la Polisi wakati wakisafirishwa kutoka Mahakama ya Mwanzo Nata kwenda Gereza la Wilaya ya Serengeti la Mugumu. Mahabusu hao walitoroka Ijumaa iliyopita majira ya saa 9:30 alasiri wakati wakisafirishwa kwa basi baada ya kufika eneo la mto Rubana likielekea mjini Serengeti. Baada ya kufika eneo hilo, basi hilo lilinusurika kupinduka kutokana na barabara kuharibika vibaya na kusababisha abiria akiwamo askari huyo kuruka ili kunusuru maisha yao. Baada ya kuteremka, inadaiwa kuwa askari huyo alijisahau hali iliyowapa nafasi mahabusu hao kutoroka na kwenda kusikojulikana na kubakia na maabusu mmoja. Hata hivyo Kamanda Polisi Mkoa wa Mara, Boaz Robert, aliliambia Nipashe kuwa mahabusu waliotoroka ni wawili na mmoja alibaki mikononi mwa askari huyo. “Tuko hilo lilitokea Ijumaa saa kumi kasorobo baada ya basi waliokuwa wamepanda kupata misukosuko ... watuhumiwa hao walitoroka wakipelekwa kwenye gereza la Mugumu, walipata nafasi ya kutoroka baada ya basi hilo la AM kunusurika kupinduka hivyo kila mmoja akawa anatoka kujinusuru, ” alisema Kamada Boazi Aliwataja mahabusu walotoroka kuwa ni Thomas Kemncha (30) ambaye alikuwa anatuhumiwa kwa kosa la shambulio na Gitati Gisemwe (20), mkazi wa Nata aliyekuwa anatuhumiwa kwa wizi. Boazi, alisema mahabusi Ndalahwa Tulami (32), mkazi wa Isenye ambaye anatuhumiwa kwa kuchoma nyumba alibaki mikononi mwa polisi na kwamba waliotoroka wanaendelea kusakwa na jeshi hilo

Brittany Murphy aaga dunia

Mcheza Sinema maarufu Brittany Murphy amefariki dunia jana. Ni yule alicheza sinema za Clueless, 8 Mile and Riding in Cars with Boys. Familia yake imesema " Tumepata pigo kubwa kwa kumpoteza mtu muhimu kwenye familia yetu , Brittany alikuwa binti mzuri, mke mzuri , mpendwa wetu na nyota kwa kila mtu“

Ndoa ya Wazazi wa BEYONCE yavunjika!!!!!!!!!!

Mama yake Beyonce, Tina Knowles, amefungua madai ya talaka mahakamani kuivunja ndoa yake na mumewe Mathew Knowles iliyodumu miaka 29.Kwa mujibu wa taarifa zilizopatikana Tina alifungua jalada la madai ya talaka kwenye mahakama moja ya Texas mwezi uliopita huku tetesi zikisema kuwa sababu ya kuvunjika kwa ndoa hiyo ni mumewe kutokuwa muaminifu na kuisaliti ndoa yao.Mathew amekuwa akitajwa sana kwenye vyombo vya habari kwa miaka kadhaa kuwa anatembea nje ya ndoa yake na hivi karibuni alifunguliwa kesi na mwanamke mmoja wa Los Angeles akituhumiwa kumpa mimba na kumtelekeza.Tina na Mathew walifunga ndoa mwaka 1980 na walizaa watoto wawili Beyonce na Solange. Wana mjukuu mmoja mwenye umri wa miaka 5.Mathew ndiye meneja wa shughuli za muziki za binti yake Beyonce wakati Tina anasimamia duka lake la nguo linaloitwa "House of Deréon" alilofungua na Beyonce mwaka 2006.Mwezi juni mwaka huu, jarida moja la udaku la Marekani liliripoti kuwa shughuli za kimuziki na biashara zimewafanya wazazi wake Beyonce waishi mbali mbali kwa muda mrefu.Beyonce akiongea katika mahojiano na jarida la Giant mwaka jana alisema kuwa amejifunza mengi kutokana na ndoa ya wazazi wake.Beyonce ambaye alifunga ndoa na rapa milionea Jay-Z mwezi aprili mwaka jana alisema kuwa amejifunza kuwa maisha ya ndoa si lelemama, wazazi wake wamekuwa wakikorofishana na kupatana mara kwa mara na kuna wakati waliishi pamoja wakati mwingine wakiishi tofauti.Mdogo wake Beyonce, Solange mwenye umri wa miaka 23, aliolewa wakati alipokuwa na umri wa miaka 17 na mchezaji soka Daniel Smith, lakini ndoa yao haikudumu sana na ilivunjika mwaka 2007.

Friday, December 18, 2009

Mungu ilaza pema Peponi Roho ya Marehemu VUMI URASA


Majonzi na huzuni vimetawala wakati wa kumuaga aliyewahi kuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya The Guardian Limited, marehemu Vumi Urasa, kwenye misa maalumu iliyofanyika Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Magomeni jijini Dar es Salaam. Urasa alifariki dunia Jumanne wiki hii kwenye Hospitali ya Hindu Mandal jijini Dar es Salaam . Baada ya mwili wake kuagwa ulisafirishwa kwenda Wilaya ya Hai mkoani Kilimanjaro kwa mazishi yatakayofanyika leo. Marehemu Urasa ameacha mke, watato watatu na mjukuu mmoja.

Achana Talaka mbele ya mashahidi

MWANAMKE mmoja [jina kapuni] jana alitoa kioja cha mwaka baada ya kupewa talaka na mumewe iliyomtaka arudi nyumbani kwao na yeye kuichana talaka hiyo mbele ya mashahidi na kuiingia ndani kwenda kulala kwa kujiamini. Mtafaruku huo ulitokea jana majira ya jioni, huko maeneo ya Magomeni Makanya baada ya mume wa mwanamke aliyetambulika kwa jina moja la Hamidu kumuandikia talaka moja mke wake huyo kwa madai kuwa alichoshwa na tabia za mke wake huyo ambaye alimuonya bila ya kujirekebisha.Hivyo Hamidu kwa kuwa alichoshwa na tabia za mke wake huyo ambaye alimkanya kwa mara kadhaa bila kumjali hivyo aliamua kuandaa mashahidi ili aweze kumkabidhi talaka hiyo kwa ushahidi.Hivyo aliandaa mashahidi wawili watatu na kuwaeleza na kumkabidhi talaka hiyo ghafla bila kuamini mwanamke huyo alipokea karatasi hiyo na alipoisoma kuwa ni talaka papohapo aliichana mbele ya watu hao na aliingia ndani kwake kwenda kulala na mashahidi hao wakibaki midomo wazi wakikosa la kusema.Akiongea na mwandishi wa habari hii mume wa mwanamke huyo alisema kuwa aliamua kumpa talaka moja mke wake huyo kwa kuwa alikuwa na tabia ya kupenda starehe na alipokuwa akitoka kwenda sehemu za starehe alikuwa anachelewa kurudi nyumbani na kurudi alfajiri kitendo ambacho alikuwa hafurahishwi nacho.Alisema yeye alikuwa anamruhusu mke wake huyo siku moja moja aende kuangalia bendi “live” lakini alikuwa anakerwa na urudiji wake wa kuchelewa na mara nyingine alikuwa akimfata sehemu husika huwa anakuwa mbishi kurudi na kutaka hadi bendi hiyo itakapotangaza kuwa wimbo huu ni wa mwisho na yeye ndiyo huanza safari ya kurudi nyumbani.“Sasa dada yangu mke wa mtu utarudiji alfajiri nyumbani kwake? Embu nisaidie, Alisema mara nyingine anaamua kumruhusu atoke peke yake kwa kuwa huwa amechoka na kumruhusu mke wake huyo atoke mwenyewe siku nyingine huwa wanatoka wote na kusema kwa kuwa mke wake huyo hupendelea sana taarabu lakini yeye hapendi sana basi ndio mana hulazimika siku nyingine amruhusu aende mwenyewe.Akiongea na chanzo chetu kwa njia ya simu mwanamke aliyepewa talaka na kuichana alipotakiwa kujibu tuhuma hizo alisema “ ni kweli nimeichana talaka mana sikuona kosa langu mimi ni nini” “halafu niende wapi na umri huu aanze yeye kuondoka kwenye nyumba ambayo tumejenga wote tukitumia mishahara yetu kwa pamoja mi sikuona kosa languAlipoulizwa kama ni kweli anachelewaga kurudi alisema ni “nadra sana, si siku zote kwanza kwa miezi miwili labda natoka maramoja tu, ujue sikia mimi mume wangu ana wivu sana sasa tunapelekana tu hivyohivyo“ yeye anachotaka mimi nikaege ndani tu bila kujiburudisha sasa akigoma akinikataza siku nyingine na mimi nikiwa na hamu ya kutoka ndipo natoka kibabe, mana yeye huwa anataka atokege yeye bila mimi sasa na mimi kitendo hicho siwezi“Mbona yeye anatoka anaenda FM Academia, Twanga nami namuacha anarudi amechelewa sanaa, na ukimwambia tutoke wote hataki namimi ndio mana naamuaga yeye akienda TWANGA mimi naenda JAHAZI

Ajifungua akifanya mazoezi Gym

Elizabeth Poblete, 22, mwanamichezo aliyeiwakilisha Chile kwenye mashindano ya kunyanyua vitu vizito kwenye olimpiki mwaka jana nchini China, amejifungua mtoto ndani ya gym alipokuwa akifanya mazoezi ya kunyanyua vitu vizito.Elizabeth alikuwa hajui kama ana mimba na alijifungua mtoto huyo kwenye gym iliyopo kwenye mji wa Sao Paulo nchini Brazili alikoweka makazi yake.Kwa mujibu wa taarifa zilizotolewa na tovuti ya habari ya Globo.com, Elizabeth alijifungua mtoto wa kiume ambaye amempa jina la Eric Jose.Akiongelea tukio hilo kocha wake wa gym, Horacio Reis, alisema kuwa alikuwa hajui kama Elizabeth alikuwa na mimba kwani wiki iliyopita aliweza kushiriki na kushinda kwenye mashindano ya kubeba vyuma yaliyofanyika nchini Chile."Mashindano yalimalizika salama na alishinda", alisema kocha wake.Kwa mahesabu ya madaktari, Elizabeth alikuwa na mimba ya miezi sita lakini kutokana na lishe na mazoezi aliyokuwa akifanya, mzunguko wake wa damu za hedhi ulikuwa hauna mpangilio maalumu hivyo kumfanya asigundue kuwa ana mimba.Elizabeth aliiwakilisha Chile kwenye mashindano ya olimpiki yaliyofanyika Beijing, China mwaka jana.Katika miezi ya karibuni, alikuwa kwenye mazoezi makali na lishe ya nguvu ili kuupandisha uzito wake kutoka kilo 75 hadi 85.

Cheka atamba kumchapa Muargentina ENRICO

Bingwa wa ngumi za kulipwa wa mikanda ya ICB na UBO, Francis "Electrified" Cheka ametamba kumtwanga mpinzani wake Enrico Areco wa Argentina katika pambano lao la litakalochezwa kesho jijini Dar es Salaam. Cheka na Areco watapanda ulingoni siku ya Jumamosi kwenye ukumbi wa PTA, kupigana katika pigano la raundi 12 kuwania taji la WBC linaloshikiliwa na Muargentina huyo na lile lake la UBO.

Mtanzania mtunisha misuli aweka Rekodi kwa kushika nafasi ya pili

MTUNISHA misuli wa Tanzania, David Nyombo(pichani) ameshika nafasi ya pili ya mashindano ya kumtafuta mtunisha misuli bora wa Afrika (Mr. Africa 2009) nchini Mauritius.
Katika mashindano hayo, mtunisha misuli wa Misri aliibuka mshindi na kuzawadiwa medali ya dhahabu huku Nyombo alizawadiwa medali ya fedha.

Ajali mbaya yatokea SAME watu 30 wahofiwa kufa

WATU zaidi ya 30 wanahofiwa kufa katika ajali nyingine mbaya iliyohusisha basi la kampuni ya Mohamed Trans ambalo liligongana uso kwa uso na basi dogo aina ya Asia Combi lililotokea eneo la Kandoto, nje kidogo ya mji wa Same mkoani Kilimanjaro. Basi hilo lenye namba za usajili T 810 AQM na ambalo lilikuwa likitokea Nairobi kwenda Dar es salaam, lililigonga basi hilo dogo ambalo inasemekana lilibeba ndugu waliokuwa wakienda Marangu kwenye harusi. Hii ni mara ya tatu katika kipindi cha miaka mitatu kwa mabasi ya kampuni ya Mohamed Trans kupata ajali mbaya iliyochukua maisha ya watu wengi, baada ya ajali iliyochukua uhai wa watu 30 mwezi Juni mwaka 2007, na ile ya Julai mwaka huu iliyotokea Korogwe, Tanga na kuchukua roho za watu 25. Hadi saa 1:00 usiku idadi ya abiria waliothibitishwa kufariki dunia ilikuwa watu 19 na karibu wote ni wale waliokuwa kwenye basi dogo aina ya Asia Combi lenye namba za usajili T 845 BCD lililokuwa likitokea Dar es Salaam kwenda Moshi. Mganga mkuu wa hospitali ya Wilaya ya Same, Dk Charles Kifunda aliithibitishia gazeti moja kuwa hadi saa 1: 00 usiku abiria 19 walikuwa wamethibitishwa kufariki ingawa taarifa nyingine zilidai kulikuwa na maiti 28 chumba cha maiti. Hata hivyo alisema kwa wakati huo haikuwa rahisi kutambua waliopoteza maisha. Basi la Asia Combi linafanya safari za daladala kati ya Sinza na Tandika jijini Dar es Salaam. Ajali hiyo ilitokea saa 10:00 jioni katika eneo la Kandoto nje kidogo ya mji wa Same mkoani Kilimanjaro katika barabara kuu ya Moshi-Dar es Salaam, eneo ambalo si hatari kwa ajali kama ilivyo maeneo mengine. Hali ilikuwa ya kutisha kwenye eneo la ajali kutokana na viungo vya watu, ikiwa ni pamoja na vichwa, miguu, mikono na ubongo kuzagaa pamoja na damu nyingi huku kukiwa na vilio kutoka kwa abiria waliojeruhiwa na wananchi ambao walikuwa wakishuhudia maiti na majeruhi hao.

Thursday, December 17, 2009

Ama kweli Mjini shule! unajua maana halisi ya Machinga? pata uhondo

Ukistaajabu ya Musa utaona ya Firauni! eti kuna tetesi kuwa hili neno la Wamachinga watu wanalielewa vibaya wabongo wengi wanafikiri kuwa wamachinga ni wale wafanyabiashara za mkononi hasahasa watu wanaotoka mikoa ya kusini, lakini ukweli ni kwamba biashara hizi hazifanywi na watu wanaotoka kusini tu ila watu wanaotoka mikoa mbalimbali katika nchi yetu

Wamachinga ni kabila mojawapo linalopatikana katika Mkoa wa lindi na jamii hii inapatikana katika maeneo ya Mchinga, mila na desturi za kabila hili hazina tofauti na watu wengine wanaotoka mikoa ya pwani.

Wabongo wengi wamelielewa Neno hili vibaya lakini kutokana na tembeatembea yangu mtaani inaonyesha walikuwa wanamaanisha (Maching - Guy) yaani wanafanyabiashara wanaofanya biashara za kutembea toka sehemu moja kwenda nyingine sasa wao baada ya kutamka Maching - Guy wanatamka Machinga ndio hapo watu wakaanza kusambaza uvumi huu na kusema wanaofanya biashar hizi ni watu kutoka kusini .


Ugumu wa maisha wamfanya auwe watu ili ahukumiwe kunyongwa

Mwanaume mmoja wa nchini China ambaye alikuwa na nia ya kujiua baada ya kushindwa kupata kazi kwa muda mrefu, amewaua watu wawili ili ahukumiwe kunyongwa. Mwanaume huyo alikuwa na nia ya kujiua lakini alikuwa hana ujasiri wa kuitoa roho yake mwenyewe. Aliamua kuwaua watu wawili ili ahukumiwe adhabu ya kunyongwa.Mwanaume huyo mwenye umri wa miaka 20 ambaye alitajwa kwa jina moja tu la Bin, alichukua uamuzi huo kutokana na hali ngumu ya maisha aliyokuwa nayo baada ya kushindwa kupata kazi kwa muda mrefu.Kwa mujibu wa vyombo vya habari vya mji wa Jiangmen katika jimbo la Guangdong, Bin aliwaua watu wawili kwa kuwanyonga ili ahukumiwe adhabu ya kifo."Bin alisema Kwa muda mrefu sina kazi, sina uwezo wa kujiua mwenyewe, nimefanya mauaji ili nihukumiwe kunyongwa", .Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na polisi, Bin hana uhusiano wowote na wala alikuwa hawajui watu aliowaua.

Mwanamke afia nyumba ya wageni Kimara

MWANAMKE ambaye hakuweza kufahamika jina wala makazi yake anayekadiriwa kuwa na umri kati ya miaka 25 na 30, amekutwa amekufa katika nyumba ya kulala wageni iitwayo Marangu huko Kimara jijini Dar es salaam. Akitoa taarifa hiyo kwa waandishi wa habari, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni, Mark Kalunguyeye, amesema tukio hilo limetokea huko maeneo ya Kimara Mwisho.Alisema maiti ya mwanamke huyo ilikutwa ikiwa imelala kitandani huku mdomoni ikiwa inatoka mapovu na haikuweza kufahamika mara moja chanzo cha kifo hicho.Alisema kuwa, mwanamke huyo alifika katika gesti hiyo Desemba 13, majira ya saa 4 asubuhi na alipanga katika nyumba hiyo akiwa na kijana mmoja aliyejitambulisha kwa jina la James Joshua, mkazi wa jijini Dar es Salaam.Katika maelezo yaliyopatikana katika nyumba hiyo ilidaiwa kuwa, kwa mara ya mwisho mwanamume huyo aliaga kwa mhudumu mmoja aliyekuwa zamu kuwa anakwenda kutafuta chakula aina ya chipsi na hakurejea tena.Amesema baada ya wahudumu kutaka kuingia katika chumba hicho kwa nia ya kufanya usafi, ndipo walipobaini dada huyo kuwa alikuwa ameshakufa.Maiti imehifadhiwa Hospitali ya Mwananyamala na polisi wanaendelea kumsaka kijana huyo kwa udi na uvumba.

Zanzibar kula christmass na giza?

Mafundi wa Kampuni ya meli maalum ya NEXANS SKAGERRAK kutoka Norway, inayoshuhulika na kazi za ulazaji wa nyaya za umeme kutoka Tanga hadi kisiwani Pemba kupitia katika bahari pamoja na mafundi wa shirika la umeme Pemba, wakitoa waya huo baharini baada ya kufikishwa Pwani ya Mkumbuu Pemba

Huyu dada anusurika kuchomwa moto kwa wizi

Mwanamke aliyejulikana kwa jina la Alejandra Maria Torres wa nchini Guatemala nchi iliyopo Amerika ya kati, akiwa pamoja na wezi wenzake watatu wa kiume, walijaribu kumchomolea pesa abiria mmoja kwenye basi lililokuwa limejaa abiria.Lakini mpango wao haukuenda vizuri, walishtukiwa katika harakati za kufanya wizi huo.Wezi wanaume walifanikiwa kukimbia na abiria walifanikiwa kumkamata Alejandra.Abiria hao wenye hasira walimvua nguo zote mwizi huyo mwanamke na kisha kumwagia mafuta ya taa kabla ya kujaribu kumchoma moto.Mwanamke huyo aliokolewa na polisi dakika ya mwisho kabla ya kuchomwa moto.

Mungu mlaze pema peponi Dk Lawrence Gama

KATIBU Mkuu wa zamani wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk Lawrence Gama amefariki dunia jana asubuhi katika Hospitali ya Aga Khan, jijini Dar es Salaam alikokuwa amelazwa kwa ajili ya matibabu. Habari ambazo Mwananchi ilizipata jana zilisema kuwa Dk Gama alikuwa akisumbuliwa na ugonjwa wa saratani. Hata hivyo, haikuweza kufahamika mara moja ni aina gani ya saratani iliyokuwa ikimsumbua kwa muda mrefu mwanasiasa huyo mwanzilishi wa CCM. Taarifa zilizopatikana jana jijini Dar es Salaam zilisema kuwa Dk Gama alikuwa akipata matibabu kwa kwenda na kurudi nyumbani katika hospitali moja, iliyoko maeneo ya Victoria jijini Dar es Salaam. Lakini, hali yake ilibadilika ghafla na kulazwa katika zahanati hiyo kabla ya kukimbizwa Aga Khan kwa matibabu zaidi ambako alifariki dunia. Chanzo cha habari kilisema kuwa hadi jana asubuhi kabla ya umauti, marehemu alikuwa akipumua kwa kutumia mashine maalumu ya hewa ya oksijeni.

Phiri wa Simba kutua leo

KOCHA wa Simba, Patrick Phiri anatarajiwa kutua nchini leo akiwa na matumaini ya kuchukua ubingwa wa michuano ya Tusker iliyoanza kutimua vumbi jana kwenye Uwanja wa Uhuru. Afisa habari wa Simba, Clifford Ndimbo alisema kuwa pamoja na kuchelewa kuja kuinoa timu hiyo kocha huyo bado ana imani kubwa na kikosi chake kufanya vizuri katika michuano hiyo.'' Ni kweli kocha amechelewa kuja baada ya kwenda likizo fupi ya ligi kuu Tanzania Bara, lakini yeye anakijua kikosi chake na anajua kuwa akiwafundisha kwa siku ngapi wanaweza kufanya vizuri hiyo ni kazi yake mwenyewe siwezi kumsemea,'' alisema Ndimbo.Aliongeza kuwa kikosi chao kimetua Dar es Salaam jana kikitokea Zanzibar walipokwenda kuweka kambi ya siku tano wakiwa chini ya kocha msaidizi Amri Said na wamejiandaa vizuri katika michuano hiyo.

Wednesday, December 16, 2009

Mungu Amlaze mahali pema peponi DJ Young Kim

MPIGA disco maarufu, Abdulhakim Magomelo (pichani) aliyekuwa akijulikana kama DJ Young Kim, alifariki jana mjini Dar es Salaam kutokana na ugonjwa wa moyo

Mtoto mdogo mwenye uwezo mkubwa wa kuogelea kuliko wote duniani

Mtoto Gibson Walker wa nchini Australia ana umri wa miezi 18 tu lakini ana uwezo wa kuogelea na kupiga raundi nne katika bwawa la kuogelea lenye urefu wa mita 25.Akifanya mazoezi katika kituo cha mazoezi ya kuogelea cha Gulliver Coomera Swim Centre, Gibson huogelea kwa mwendo kobe wa taratibu lakini hufanikiwa kumaliza raundi nne kuzunguka bwawa la kuogelea bila kupumzika.Baba yake Gibson, Mark alisema kuwa alianza kumfundisha mwanae kuogelea tangia alipokuwa na umri wa miezi sita na ghafla alianza kupenda kuogelea."Anajiamini sana anapoogelea kiasi cha kunifanya nisiwe na hofu yoyote", alisema baba wa mtoto huyo.Mafunzo ya kuogelea aliyopewa akiwa na umri mdogo yalimsaidia mtoto huyo kuokoa maisha yake wakati alipodondoka pembeni ya bwawa la kuogelea na kuangukia kichwa kabla ya kuangukia kwenye bwawa la kogelea.Gibson badala ya kuanza kulia kama watoto wenzake ambavyo wangefanya, aliogelea hadi kwenye ukingo wa bwawa hilo na kujitoa mwenyewe nje ya bwawa hilo ndipo akaanza kulia.Mwalimu wake wa kuogelea Terry Gulliver ana rekodi nzuri ya kuwafundisha watoto wenye umri mdogo kuogelea. Aliwahi kumfundisha mtoto wa miaka mitatu kuweza kuogelea mita 1500 bila matatizo yoyote."

Dunia Imeisha - Mtawa Kortin kwa Utapeli!!!!!

MTAWA wa Kanisa Katoliki Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Angela Singira (pichani), amefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kinondoni jijini Dar es Salaam kujibu mashtaka matano tofauti ya kujipatia mali kwa njia ya udanganyifu. Kesi hizo zilisomwa jana mahakamani hapo na waendesha mashtaka mbalimbali mbele ya mahakimu wakazi wanne tofauti. Mwendesha mashtaka wa polisi Inspekta Boniface Edwin alimwambia Hakimu Ferdinand Kiwonde katika hati ya kwanza ya mashtaka kuwa, kati ya Aprili 10 na 20 mwaka huu, saa 3:00 asubuhi maeneo ya Bunju 'A', jijini Dar es Salaam, mtuhumiwa alijipatia mkopo wa vitu mbalimbali vyenye thamani ya Sh 625,000 kwa njia ya udanganyifu. Alisema mtuhumiwa huyo alijipatia mkopo huo kutoka kwa Isaya Rafael baada ya kujifanya wakala wa shule ya Sekondari ya Cornelius. Kwa mujibu wa mwendesha mashtaka huyo baada ya kujitambulisha hivyo, alichukua mboga za majani na viungo akieleza kuwa anawapelekea wanafunzi wa shule hiyo. Katika kesi ya pili, mtuhumiwa huyo anakabiliwa na shtaka la kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu. Mwendesha mashtaka wa polisi Mohamed Kilongo alimwambia Hakimu Jackline Rugemalila kuwa Agosti 9 mwaka huu, saa 3:00 asubuhi maeneo ya Kinondoni, mtuhumiwa alijipatia Sh 250, 000 kutoka kwa Joackim Peter. Aliieleza mahakama kuwa katika shtaka la tatu mtuhumiwa huyo anakabiliwa na kesi ya kujipatia mkopo kwa kutumia nguvu. Kilongo alimwambia tena Hakimu Rugemalila kuwa Februari 5 mwaka huu saa 4:00 asubuhi maeneo ya Tegeta Machinjioni, mtuhumiwa alijifanya wakala wa Shule ya Sekondari ya Cornelius na kujipatia mkopo wa vitu vyenye thamani ya Sh 480, 000. Alisema baada ya utambulisho huo, alichukua kilo100 za mchele, maharage kilo 100, sukari kilo 25, unga wa mahindi kilo 50 na mikate 200 kutoka kwa Hassan Mahmud. Katika shtaka lingine mwendesha mashtaka huyo alisema bila kutaja jina lake la kwanza, Januari Mosi mwaka huu saa 5:00 asubuhi maeneo ya Salasala, jijini Dar es Salaam mtuhumiwa alijifanya wakala wa shule hiyo na kujipatia mkopo wa kilo 90 za maharage zenye thamani ya Sh117,000 kutoka kwa Christopher Bondi. Hati ya mashtaka pia imeeleza kuwa katika kesi ya tano mtuhumiwa huyo alijipatia mkopo wa vitu vyenye thamani ya Sh380,000 kwa njia ya udanganyifu. Mwendesha mashtaka wa polisi Inspekta Idd Kiwogoma alimwambia Hakimu Sundi Fimbo kuwa mtuhumiwa huyo alitenda kosa hilo baada ya kujifanya wakala wa shule hiyo ya sekondari na kuchukua mikate 130 kutoka kwa Haruna Issa. Hata hivyo, mtuhumiwa huyo alikana mashtaka hayo yote na kesi hiyo kuahirishwa hadi Desemba 29, mwaka huu itakapotajwa tena. Dhamana ya mtawa huyo ilikuwa wazi, lakini hakupata mdhamini hivyo alipelekwa rumande.

Tuesday, December 15, 2009

Simba haitikisiki na mkwala wa TFF

Uongozi wa klabu ya Simba umesema haustushwi na tishio la Shirikisho la Soka nchini (TFF), kwamba hawatashiriki michuano ya Kombe la Shirikisho Afrika kutokana na kuchelewesha kupeleka majina ya usajili wa wachezaji kwasababu wanaifahamu tarehe ya mwisho ya zoezi hilo kuwa ni leo. TFF ilizitaka klabu za Simba na Yanga, inayoshiriki michuano ya Ligi ya Klabu Bingwa Afrika, kuwakilisha majina ya usajili wa wachezaji wao watakaoshiriki michuano hiyo inayosimamiwa na Shirikisho la Soka Afrika, CAF, Jumamosi iliyopita, ambapo Yanga ilitekeleza lakini Simba waliomba waongezewe muda wa siku moja ili kukamilisha jambo hilo. TFF iliipa muda huo Simba na kuitaka iwe imekamilisha zoezi hilo juzi Jumapili. Hata hivyo, pamoja na kuongezewa muda huo bado uongozi wa Simba ulishindwa kutekeleza agizo hilo hali iyosababisha Katibu Mkuu wa TFF, Fredrick Mwakalebela kuwataka viongozi hao kutekeleza agizo akisisitiza kuwa watakosa michuano hiyo endapo hawatawasilisha majina hayo. Licha ya tishio hilo kutoka TFF, Simba ilishindwa kuwasilisha majina hayo kwa madai kuwa hailitambui agizo la TFF na kwamba wao wanaangalia tarehe ya mwisho ya kuwasilisha majina iliyowekwa na CAF ambayo ni leo Desemba 15. Akizungumza na vyombo vya habari jana, Afisa Habari wa klabu hiyo, Cliford Ndimbo alisema kuwa wanachojua wao ni kuwa siku ya mwisho ya kuwasilisha majina ya wachezaji wao CAF ni leo na si Jumamosi iliyopita kama ilivyotangazwa na TFF. "Hilo agizo la TFF hatulitambui, tunachokijua ni kuwa mwisho wa kuwasilisha majina CAF ni kesho (leo), sasa hayo masuala mengine sisi hatuyapi nafasi kwa sababu tunafanya kazi kwa taratibu tulizojiwekea," alisema Ndimbo. Hata hivyo, alieleza kuwa jana waliwasilisha majina 27 ya wachezaji wao watakaoshiriki michuano hiyo, ambapo katika orodha ya wachezaji wao wote waliowasajili wamewaacha George Nyanda, Adam Kingwande na Meshack Abel ambao wamesajiliwa African lyon kwa mkopo. Lakini Nipashe ilipomuuliza Mwakalebela kama majina ya wachezsaji wa Simba yamefika, alijibu kwa kifupi kuwa bado hawajayawasilisha kwenye ofisi yake. Kwa upande mwingine Ndimbo alisema kuwa timu yao inatarajia kurejea leo kutoka Zanzibar ilikoeweka kambi kwa ajili ya kujiandaa na michuano ya Kombe la Tusker ambapo keshokuitwa wataanza mazoezi chini ya kocha wao Patrick Phiri anayetarajia kurejea leo kutoka mapumzikoni nchini Zambia.

Papic akiri kikosi cha Yanga bado ni dhaifu kinahitaji marekebisho

Kocha wa Yanga, Kostadin Papic amesema kuwa kikosi chake bado ni dhaifu na anahitaji kukifanyia marekebisho ya haraka kabla ya kuanza harakati za kuwania Kombe Tusker inayotarajiwa kuanza leo, jijini Dar es Salaam. Yanga inatarajia kuanza mshike mshike wa kuwania ubingwa wa michuano hiyo Ijumaa kwa kumenyana na Mafunzo ya Zanzibar. akizungumza na vyombo vya habari jana, Papic alisema kuwa hajaridhishwa na kiwango kilichoonyeshwa na timu yake kwenye mchezo wao wa kirafiki dhidi ya TMK United, ambapo mabingwa hao watetezi wa ligi kuu nchini walikubali kipigo cha magoli 2-0. Papic alieleza kuwa mchezo dhidi ya TMK ulimsaidia kuona udhaifu wa timu yake, ambapo ili kuhakikisha wanatoa ushindani kwenye michuano hiyo wanahitaji mabadiliko ya haraka kabla ya kuingia uwanjani. "Nimeona timu yangu bado ni dhaifu, licha ya kwamba nyota wetu tisa walikuwa hawajarudi (kutoka kuziwakilisha timu zao za taifa katika michuano ya Chalenji nchini Kenya), na inahitaji marekebisho ya haraka ili kuhakikisha tunashindana kwenye michuano ya Tusker, sitaki tuwe washiriki, nataka tuwe washindani," alisema Papic. Aliongeza kuwa anaamini mabadiliko hayo yatafanyika mara baada ya wachezaji wake wote kurejea kwenye timu mara baada ya kumaliza majukumu ya timu zao za Taifa. Aliweka wazi kuwa timu kuwakosa zaidi ya wachezaji sita ni pengo kubwa ambalo linaweza kuiathiri timu kama ilivyotokea kwenye mchezo wao dhidi ya TMK. Papic aliongeza kuwa udhaifu mkubwa aliouona kwenye timu yake ni safu ya ulinzi ambayo imekosa kuelewana pale tu timu inaposhambuliwa huku washambuliaji wake wakishindwa kulijua jukumu lao wanapokuwa na mpira.

Mikakati au Kampeni zimeanza?

Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe akiwa anahutubia mkutano wa operesheni Sangara juzi katika uwanja wa Tangamano mjini Tanga na kuwataka wakazi wa mji huo kujipanga kwa uchaguzi mkuu ujao kufanya mabadiliko

Je vitu hivi vinapelekwa wapi ofisini au?

Askali Mgambo wa Halmashauri ya Ilala akisukuma toroli lililojaa mananasi baada ya kunyang'anya kwa muuzaji aliyekuwa akifanya biashara katika eneo lisiloruhusiwa mtaa wa Sikukuu jijini Dar es Salaam

Kesi ya akina Mramba kusikilizwa siku 3 mfululizo

Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam, leo itaendelea kumsikiliza shahidi wa tatu kwenye kesi ya matumizi mabaya ya madaraka na kuisababishia serikali hasara ya Sh. bilioni 11.7 inayowakabili mawaziri wawili wa zamani, Basil Mramba, Daniel Yona na Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Gray Mgonja. Kesi hiyo inasikilizwa na jopo la mahakimu watatu wakiongozwa na Mwenyekiti John Utamwa, Saul Kinemela na Sam Rumanyika, itasikilizwa kwa mfululizo hadi Desemba 18, mwaka huu. Awali, mahakama hiyo ilisikiliza mashahidi wawili na iliahirishwa hadi shahidi wa tatu atakapotoa ushahidi wake. Katika kesi hiyo, washtakiwa wanadaiwa kuwa kati ya Agosti mwaka 2002 na Juni 14, mwaka 2004, jijini Dar es Salaam, wakiwa watumishi wa umma kama mawaziri na katibu mkuu walitumia vibaya madaraka. Ilidaiwa kuwa kwa kupitia kampuni ya Alex Stewart (Assayers) ya Uingereza iliyoingia mkataba wa ukaguzi wa madini kupitia kampuni tanzu ya Alex Stewart (Assayers) Government Business Corporation waliingia mkataba kukagua kiwango cha uzalishaji wa madini ya dhahabu kinyume cha Sheria ya Manunuzi ya Umma. Awali shahidi wa kwanza Nyelo Godwin (48) alidai mahakamani hapo kwamba mkataba wa kampuni ya Alex Stewart ulipitishwa licha kuwepo kwa mapendekezo ya kuuzuia usisainiwe. Pia, alidai kuwa kati ya asilimia 3 ya fedha zilizokuwa zinapatikana kwa mwaka, kampuni hiyo ilikuwa inalipwa asilimia 1.9 na serikali ilibaki na asilimia 1.1. Naye shahidi wa pili, Betha Soka (44) alidai kwamba Yona alimdanganya Rais wa awamu ya tatu kwa kumpelekea taarifa kwamba majadiliano ya mchakato wa kuipa kazi ya ukaguzi wa madini Kampuni ya Alex Stewart yalishirikisha ofisi ya Mwanasheria Mkuu. Soka alidai kupitia dokezo lililoandikwa na mshitakiwa wa pili Yona, kwamba majadiliano ya mchakato huo yalifanywa kwa pamoja kwa kuhusisha wizara ya Nishati na Madini, Wizara ya Fedha, Benki Kuu Tanzania (BoT) na ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na alimjulisha Rais Mkapa kuwa yanaendelea vizuri.

BOT yamwaga Mikopo kwa Wafanyakazi wake

MILANGO ya neema imefunguka kwa wafanyakazi wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT). Kila mfanyakazi ataweza kukopa kati ya Sh 100milioni na Sh 30milioni kulingana na wadhifa wake kwa ajili ya ujenzi wa nyumba. Habari ambazo Mwananchi imezipata zinasema kwamba mikopo hiyo itatolewa katika madaraja manane. Viwango hivyo vya mikopo ni vipya ambavyo vimetokana na maombi ya wafanyakazi hao ya kuongezewa kiasi cha mikopo hiyo kutoka katika kiwango cha awali walichokuwa wakipewa. Wafanyakazi wa daraja la chini kabisa, watakuwa wanakopeshwa Sh30milioni, wakati wafanyakazi wa ngazi ya juu kabisa watapata mkopo wa Sh100milioni. Wafanyakazi wa daraja la kwanza ambalo ni la juu kabisa na ambao watakuwa wanapata mkopo huo wa Sh100milioni ni pamoja na wakurugenzi, wakurugenzi washiriki na wataalamu washauri waandamizi. Daraja la pili ni la wafanyakazi wenye vyeo vya mameneja na wataalamu washauri ambao watapata mkopo wa Sh90milioni, wakati daraja la tatu linawahusisha mameneja wasaidizi na maafisa wakuu waandamizi (professional I) ambao wao watapata mkopo wa Sh70milioni. Daraja la nne linawahusisha wafanyakazi wenye vyeo vya maafisa wakuu (professional I) na maafisa wakuu waandamizi (professional II), ambao wao watajipatia mkopo wa Sh 60milioni, huku wafanyakazi katika daraja la tano ni wale wenye vyeo vya maafisa waandamizi (professional I) na maafisa wakuu (professional II) ambao watajipatia mkopo wa Sh 55milioni. Katika daraja la sita kuna wafanyakazi wenye vyeo vya maafisa ngazi ya III-I (professional I), maafisa waandamizi (professinal II) na maafisa- makarani wakuu (cleric officers) ambao watajipatia mkopo wa Sh45milioni. Daraja la saba ni la wafanyakazi wenye vyeo vya maafisa-makarani kuanzia ngazi ya III hadi ngazi ya maafisa-makarani waandamizi (cleric officers), makarani waandamizi na makarani wakuu (clerks) ambao wao watajipatia mkopo wa Sh40milioni. Daraja la nane ambalo ni la chini kabisa linawahusisha wafanyakazi wa taasisi hiyo ambao ni walinzi, wapishi, madereva, wahudumu wa ofisi na wa zahanati na makarani ngazi ya daraja la III-I ambao watapata mkopo wa Sh30milioni. Habari hizo zinasema kwamba viwango vya awali kwa wafanyakazi wa daraja la kwanza na la pili kama ilivyoainishwa hapo juu vilikuwa ni Sh50milioni, daraja la tatu vilikuwa Sh35milioni, daraja la nne na la tano Sh30milioni. Katika daraja la sita viwango vya awali vilikuwa ni Sh25milioni, daraja la saba walikuwa wakipata mkopo wa Sh20milioni wakati daraja la nane ambalo ni la chini walikuwa wakipata mkopo wa Sh15milioni. Kwa mujibu wa waraka uliosainiwa na Naibu Mwenyekiti wa Mfuko wa Mikopo ya Nyumba, Len Kisarika kwenda kwa wafanyakazi wote wa makao makuu na katika matawi ya Mwanza, Arusha, Mbeya, Zanzibar na Chuo cha Benki Mwanza kuwafahamisha kuridhia nyongeza hiyo, menejimenti hiyo imeridhia nyongeza hiyo ya mikopo ili kukidhi ongezeko la gharama za ujenzi. Katika waraka huo wa Desemba 2, mwaka huu ambao nakala yake imepelekwa kwa Gavana wa BoT, Profesa Beno Ndullu na kwa Manaibu Gavana, menejimenti hiyo pia imeidhinisha ongezeko la kiwango cha mkopo kwa ajili ya matengenezo ya nyumba kutoka asilimia 15 hadi 20 ya mkopo uliotolewa. Waraka huo pia unabainisha kuwa kufuatana na hali ya Mfuko wa Mikopo ya Nyumba na ili kuhakikisha kuwa mikopo inayotolewa inatumika kwa malengo yaliyokusudiwa, utoaji wake umefanyiwa marekebisho kutegemea vipaumbele na masharti mbalimbali. Kwa mujibu wa waraka huo, kipaumbele cha kwanza ni kwa waombaji wapya, cha pili ni maombi ya nyongeza ya mikopo kwa ajili ya nyumba ambazo bado hazijakamilika na kipaumbele cha tatu ni maombi ya nyongeza ya mikopo kwa ajili ya uboreshaji wa nyumba. Masharti yaliyotajwa katika waraka huo kwa kipaumbele cha kwanza ni pamoja na salio la theluthi moja ya mshahara wa mwombaji baada ya makato, kama ilivyoainishwa kwenye Sheria ndogo za utumishi za (BoT Staff By Laws, 2008), uwezo wa mkopaji kurejesha mkopo na kuwasilisha hati ya kiwanja ambayo haijatolewa kama dhamana na isiyo na kikwazo chochote. Katika kipaumbele cha pili na cha tatu, mbali na masharti yanayotajwa katika waraka huo pamoja na masharti ya kwenye kipaumbele cha kwanza, kuna nyongeza ambayo ni pamoja na ukaguzi wa nyumba husika itakayofanyiwa uboreshaji kwa kipaumbele cha tatu. Masharti mengine ya kipaumbele cha pili ni ukaguzi wa nyumba husika ili kuthibitisha hatua iliyofikia katika ujenzi, tathmini ya thamani ya nyumba husika kutoka kwa mthamini wa majengo aliyesajiliwa, tathmini ya kamati ya kuthibitisha kama kiasi cha mkopo kinachoombwa kama kinatosheleza kukamilisha ujenzi wa nyumba husika.

Monday, December 14, 2009

Gari ya Mashindano laua watoto 5


WATU watano wamekufa, kati yao wanne papo hapo, baada ya gari la mashindano ya mbio za magari kuacha barabara na kuparamia umati wa watu waliojipanga kando kando ya njia eneo la Mikese Njianne, wilayani Morogoro. Ajali hiyo imesababisha pia majeruhi 12 ambao wamelazwa katika Hospitali ya Mkoa wa Morogoro. Gari hilo lenye namba za usajili kutoka Kenya KAK 9208 aina ya Subaru likiwa miongoni mwa magari 16 yaliyoshiriki, liliandikishwa namba sita ya katika mashindano ya mbio za umbali wa kilometa 380 yajulikayo kwa jina la Morogoro Pathfinder Rally 2009 na iliendeshwa na dereva Dharam Pandya( 29). Kaimu Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Morogoro, Ferdinand Mtui, alithibitisha kuwa ajali hiyo ilitokea jana saa 4:30 asubuhi eneo la Mikese Njianne kwenye barabara ya vumbi. Kwa mujibu wa Kaimu Kamanda huyo, watu waliokufa kwenye ajali hiyo ni watoto wenye umri kati ya miaka sita na kuendelea waliokuwa miongoni mwa watazamaji wa mashindano hayo. Alisema ajali hiyo katika barabara ya vumbi mara baada ya kufika Mikese Mizani, ambapo magari hayo yalitumia barabara ya kawaida na gari hilo lilipofika eneo lenye kona liliacha njia na kuwaparamia watu na kupinduka na hivyo kusababisha vifo hivyo na majeruhi hao. Kati ya maiti hizo nne mmoja ndiye iliyotambuliwa kwa jina la Jacob Mashaka ( 6) ambaye ni mwanafunzi wa Shule ya Awali katika Kijiji cha Mikese. Naye Ofisa wa zamu katika Hosptitali ya Mkoa wa Morogoro, Judith Kagimbwa, alithibitisha kupokea majeruhi 12 na miili minne. Alisema majeruhi mwingine alifariki akiwa wodini saa 7:30 mchana. Naye ni Said Mohamed ( 40) . Majeruhi 11 wanaoendelea kupatiwa matibabu ni Pamela Ashumba ( 50), Mgema Deus (16), Mwanaidi Rajab (21), Iddi Hamis ( 40), Hadija Mwarabu (28), Mwamini Said (28), Juma Abdallah (33), Alex Mussa (14) Daniel Masanja (12) na Shukuru Roma (28) ambao baadhi yao ni wakazi wa Mikese na wengine nje ya Mikese.

Secretary wa Ubalozi aliwatemea Mate Polisi na Muandishi wa Habari arudishwa kwao!!!

OFISA wa Ubalozi wa Canada nchini, Jean Touchatte (48) aliyemtemea mate askari wa usalama barabarani na mwandishi wa habari kwa nyakati tofauti, amerudishwa nchini kwao. Touchatte aliwatemea mate watumishi hao wa umma Jumatano iliyopita, Dar es Salaam. Ubalozi wa Canada umemuamuru aondoke mara moja, na nchi hiyo imeeleza kusikitishwa na kitendo hicho. Taarifa ya ubalozi iliyotolewa jana Dar es Salaam, imesema, “tunasikitika kwa tukio la Jumatano, Desemba 9 likihusisha mmoja wa maofisa wetu.”Touchatte alikuwa Katibu Muhtasi wa ubalozi. Ubalozi huo umesema, kwa faida ya pande zote, umeona ni vyema ofisa huyo aondoke mara moja na arudi Canada. Touchatte alimtemea mate Koplo Samson na baadaye akafanya hivyo kwa Mwandishi wa habari, Jerry Muro (29) wa Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC). Muro amesema, hakubaliani na hatua ya ubalozi kumwondoa nchini kabla ya kufikishwa katika vyombo vya sheria. Amesema, ataendelea kufuatilia ili kuhakikisha kwamba mtuhumiwa huyo anaadhibiwa kisheria. “Sikubaliani. Lazima haki itendeke. Kumfukuza ni hatua mojawawapo, lakini haimaanishi kwamba yamekwisha. Nitakwenda polisi wazuie hati yake ya kusafiri,” amesema Muro.

Kili Stars Yawasili Na Mfungaji Bora Wa Chalenji

BAADA ya kushindwa kutwaa ushindi wa tatu wa michuano ya Kombe la Chalenji, timu ya taifa ya Tanzania Bara ‘Kili Stars’ inatarajiwa kuwasili nchini mchana huu ikitokea Kenya. Kwa mujibu wa habari kutoka kwa Katibu Mkuu wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Frederick Mwakalebela, alisema timu hiyo itawasili mchana huu katika Uwanbja wa ndege wa Julius Nyerere.“Tunaomba wadau wajitokeze kuja kuipokea timu yetu ya taifa, lengo ni kuwapa hamasa wachezaji wetu kwa maendeleo ya zoka letu,” alisema Mwakalebela.Kili Stars inawasili na mfungaji bora wa Kombe la Chalenji Mrisho Ngassa aliyefunga mabao matano.

Kikongwe cha miaka 98 chaau kikongwe cha miaka 100

Bibi mwenye umri wa miaka 98 wa nchini Marekani amefunguliwa mashtaka ya mauji kwa kumuua bibi mwenye umri wa miaka 100 aliyekuwa akiishi naye chumba kimoja kwenye nyumba ya kutunza vikongwe. Bibi Laura Lundquist mwenye umri wa miaka 98 anakabiliwa na kesi ya mauaji ya bibi mwenzake mwenye umri wa miaka 100. Bibi Laura anatuhumiwa kumziba pumzi mpaka kumuua bibi Elizabeth Barrow aliyekuwa akiishi naye chumba kimoja kwenye nyumba ya kutunza vikongwe iliyopo Massachusetts nchini Marekani. Jaji wa kesi hiyo ameamuru bibi Laura apelekwe hospitali kwanza kupimwa akili zake kabla kesi hiyo haijaendelea. Katika tukio hilo lililotokea septemba 24, Bibi Elizabeth alikutwa amefariki chumbani kwake huku mfuko wa plastiki ukiwa juu ya kichwa chake. Mtoto wa kiume wa bibi Elizabeth, Scott Barrow alisema kuwa bibi Laura alikuwa akimtishia maisha mama yake mara kadhaa alipokuwa akimtembelea kwenye nyumba hiyo.

Majaji Miss Tanzania angalieni vigezo upya la sivyo itakuwa ni watu wa kusindikiza kila siku

Miss Dunia mwaka 2009 Kaiane Aldorino

MASHINDANO ya kumtafuta mrembo wa dunia yamefanyika jana huko Johannesburg, Afrika Kusini huku mrembo wa Tanzania akitoka mikono mitupu katika mashindano hayo. Katika mashindano hayo mwaka huu Tanzania iliwakilishwa na mrembo Miriam Gerald, ambaye amekuwa ni mrembo wa 16 wa Tanzania kuwania taji hilo tangu mwaka 1994. Mrembo Nany Sumari ndiye pekee aliyeweka rekodi nchini kwa kuibuka na taji la Afrika au Miss World Africa mwaka 2005 kwa kuwa miongoni mwa warembo watano bora duniani. Mashindano hayo ya 59 ya kumtafuta mrembo wa dunia mwaka huu yalishirikisha warembo 112, ambapo mrembo kutoka Gibraltar anayeitwa Kaiane Aldorino ndiye aliyeibuka mshindi. Tunapenda kumpongeza Miriam kwa kujitahidi kuliwakilisha Taifa ingawa hakufanikiwa kufanya vizuri katika mashindano hayo. Tunatarajia waandaaji wa Miss Tanzania watakuwa wamejiunza mengi katika mashindano hayo ya dunia na watajitahidi kuboresha mashindano yetu.

Jamani hii ni kukwepa Foleni au?


Waziri Mkuu wa Italia apigwa na kutolewa meno 2


Waziri mkuu wa Italia Silvio Berlusconi amekumbana na kitu asichokitegemea maishani mwake baada ya kushushiwa kipigo mtaani kilichobabisha apoteze meno mawili. Mwanaume mmoja anashikiliwa na polisi nchini Italia baada ya kumshambulia waziri mkuu wa nchi hiyo Silvio Berlusconi na kumjeruhi usoni na kupelekea meno yake mawili yang'oke.Katika tukio hilo lililotokea jana jumapili asubuhi, wasaidizi wa Berlusconi mwenye umri wa miaka 73 waliwahi kumuokoa bosi wao asijeruhiwe zaidi na walimwahisha kwenye gari lake huku akivuja damu usoni. Aliwahishwa hospitali ambako anatarajiwa kukaa kwa masaa 24."Niko poa , niko poa", alinukuliwa akisema Berlusconi na shirika la habari la ANSA wakati alipokuwa akitoka kwenye chumba cha dharura cha hospitali.Mwanaume aliyemshambulia alikamatwa na kupelekwa makao makuu ya polisi ya mjini Milan.Taarifa zilizotolewa baadae zilisema kuwa mwanaume huyo alikuwa na historia ya matatizo ya akili kwa miaka 10.Waziri wa ulinzi Ignazio La Russa, ambaye alikuwa karibu na Berlusconi wakati wa shambulio hilo alisema kuwa waziri mkuu alikuwa akivuja damu puani na mdomoni. ANSA lilimkariri mmoja wa madaktari akisema kuwa meno mawili ya Berlusconi yaling'oka katika shambulio hilo.Berlusconi alikumbwa na zahama hilo wakati wa maandamano ya kisiasa yaliyofanyika jijini Milan.Berlusconi alikumbwa na tukio kama hilo miaka michache iliyopita wakati kijana mmoja mdogo alipomshambulia kwa kumpiga na chuma la stendi ya kamera na kusababisha apate jeraha kichwani kwake.Berlusconi amekuwa kwenye presha kubwa kuhusiana na maisha yake binafsi na maisha yake ya kisiasa akishutumiwa kufanya ubadhirifu serikalini.Pamoja na shinikizo hilo, Berlusconi, ambaye alishinda uchaguzi mwezi mei mwaka jana amesisitiza kuwa hataitisha uchaguzi mapema kabla ya muda wake.

Tiger Wood kustaafu kucheza Golf?

Nyota namba moja duniani wa mchezo wa gofu, Tiger Woods amekiri kuisaliti ndoa yake na ameamua kustaafu kwa muda kucheza gofu baada ya wanawake 11 wakiwemo wacheza filamu za ngono kujitangaza kufanya naye mapenzi. Tiger Woods ameamua kustaafu kwa muda usiojulikana kucheza mchezo wa gofu baada ya idadi ya wanawake aliofanya nao mapenzi nje ya ndoa kuzidi kuongezeka.Jumla ya wanawake 11 wameishajitokeza na kujitangaza hadharani kuwa walifanya mapenzi mara kadhaa na nyota huyo maarufu duniani kwa mchezo wa gofu.Katika ujumbe aliouandika katika tovuti yake, Tiger Woods amekiri kuisaliti ndoa yake na amemuomba radhi mkewe Elin Nordegren kwa fedheha aliyomsababishia.Woods alisema kuwa anaamua kustaafu gofu kwa muda usiojulikana ili aweze kujishughulisha na familia yake akijifunza kuwa mume na baba mzuri.Hatua hiyo ya Woods imekuja kufuatia taarifa kuwa Woods alikuwa akitumia maelfu ya dola kuwahonga makahaba ghali wakati alipokuwa akishiriki kwenye matamasha ya gofu sehemu mbali mbali duniani.Taarifa zilisema kwamba ni mara chache sana Woods alichukua kahaba mmoja. Alikuwa akipenda kuona wanawake wakisagana hivyo karibia mara zote alikuwa akiwachukua makahaba wawili wawili.Woods pia amekuwa katika zengwe na Wamarekani weusi kufuatia madai kuwa alikuwa akipenda kujifanya mzungu na hakupenda wanawake weusi na ndio maana katika wanawake wote 11 waliojitokeza hakuna hata mwanamke mmoja mweusi.Woods amebaki peke yake hakuna nyota yoyote mweusi aliyemtetea huku baadhi ya madj katika redio za Marekani wamekuwa wakitoa maneno na rap za kebehi dhidi yake.Tiger, ambaye ana watoto wawili aliozaa na mkewe Elin, maisha yake ya ngono za siri akimsaliti mkewe yaligundulika kufuatia ajali isiyotegemewa nje ya nyumba yake.Katika ajali hiyo, Tiger Woods akiendesha gari lake kutoka nyumbani kwake kwenye majira ya saa nane usiku aligonga mti na kuzimia kwenye eneo la ajali hiyo.Taarifa zilizotolewa baadae zilisema kwamba Tiger Woods aliligongesha gari lake alipokuwa akimkimbia mkewe kufuatia mzozo wa mahusiano yake na mmoja wa wapenzi wake wa siri.Wadhamini wa Tiger Woods kama vile Pepsi, Gillette na Proctor and Gamble wapo kwenye majadialino ya kuendelea kumdhamini Woods au kumtosa.

Friday, December 11, 2009

Mashoga Uganda Kuhukumiwa Adhabu ya Kifo?

Wakati Marekani baadhi ya majimbo yanaruhusu ndoa za jinsia moja, Mashoga watakaokamatwa nchini Uganda watahukumiwa adhabu ya kifo na familia zao zitatupwa jela miaka saba iwapo zitashindwa kuwafichua hadharani huku wenye nyumba watakaowapingasha nyumba zao mashoga nao huenda wakanyea kwenye makopo ya jela. Hayo yamo katika muswada mpya wa sheria ya kupambana na ushoga nchini Uganda ambao uko njiani kupitishwa kuwa sheria.Muswada huo umezua mtafaruku katika jamii ya mashoga duniani na leo alhamisi maandamano ya mashoga wa Uingereza yanafanyika jijini London kuupinga muswada huo.Mwezi uliopita mashoga wa Marekani waliandamana kuupinga muswada huo ambao Uganda imesisitiza itaupitisha pamoja na shinikizo kubwa toka mataifa wafadhili.Watetezi wa haki za mashoga na wasagaji wamedai kuwa muswada huo utarudisha nyuma juhudi za kupambana kuzuia kuenea kwa ukimwi. David Cato(pichani), shoga ambaye aligeuka kuwa mtetezi wa mashoga baada ya kupewa kipigo mara nne, kutiwa mbaroni mara mbili na kufukuzwa kazi kwasababu ya ushoga wake, alisema: "Wakati tulipojitokeza kudai haki zetu ndio wameamua kutunga sheria dhidi yetu".Cato pamoja na wanaharakati wenzake wa kutetea haki za mashoga na wasagaji wanahofia muswada huo utapitishwa kuwa sheria. Hata hivyo baadhi ya raia wa Uganda wanauunga mkono muswada huo ili kukomesha tabia ya ushoga na usagaji ambayo imekuwa ikukua kwa kasi katika miaka ya hivi karibuni."Vijana wa sekondari wanaiga kila kitu toka nchi za kimagharibi na Marekani", alisema mwalimu wa sekondari David Kisambira ambaye anaunga mkono muswada huo."Kuna idadi kubwa ya wanafunzi wamegeuka kuwa mashoga na wasagaji, tunasikia kuwa kuna vikundi vya watu vinavyopewa pesa na taasisi za mashoga katika nchi zilizoendelea, zinaajiri vijana na kuwaingiza katika shughuli za kishoga", alisema mwalimu huyo.Kisambira kama walivyo viongozi wengi wa Uganda wanataka sheria kali zitungwe ili kutokomeza suala hilo.

Mtuhumiwa wa Mauaji ya mkewe mtarajiwa na mama mkwe atoroka akiwa chini ya ulinzi wa polisi

Mtuhumiwa wa mauaji ya watu wawili na yeye kujaribu kujichinja koromeo ametoroka akiwa katika hospitali teule ya DDH, Serengeti, huku akiwa chini ya ulinzi. Mtuhumiwa huyo ametoroka wakati akiwa amepewa rufaa kwenda Bugando kwa matibabu. Tukio hilo linadaiwa kuwa ni la pili kwa askari magereza kutorokwa na mtuhumiwa wa mauaji hapo hospitali, hali ambayo inaibua maswali mengi huku uongozi wa jeshi hilo ukiwa kimya. Habari za uchunguzi zimebaini kuwa Muyuga Maduhu (25), mkazi wa kijiji cha Rigicha aliyekuwa anakabiliwa na mashitaka ya kuwaua watu wawili; mama mkwe wake mtarajiwa, Mageni Masaka (60) na mchumba wake, Suzana Chande Makanika (30) kwa kuwakatakata kwa panga kutokana na wivu wa mapenzi, alitoroka hospitalini hapo akisubiri kupelekwa Bugando kwa matibabu zaidi. Mshitakiwa huyo ambaye tayari alikuwa ameshasomewa mashitaka mawili ya mauaji akiwa kitandani alikabidhiwa kwa askari magereza baada ya kusomewa mashitaka na alikuwa chini ya uangalizi wao kwa muda wote. Habari kutoka vyanzo vya habari hospitalini hapo zimedai kwamba Maduhu anayedaiwa kutenda unyama huo Novemba 4, mwaka huu, saa 7:00 usiku, alisomewa mashitaka Novemba 6 kisha akakabidhiwa kwa askari magereza ambao walikuwa wakipeana zamu kumlinda na inaelezwa kwamba muda wote alikuwa amefungwa pingu kitandani. Inaelezwa kwamba wakati muda wote Maduhu alikuwa kwenye pingu hata anapokwenda chooni, siku ya tukio askari aliyekuwa akimlinda alimfungua pingu zote na kumwacha aende pekee yake chooni. Inasemekana kwamba askari huyo, jina tunalo, alikuja kushtuka baadaye kwamba hamuoni mshitakiwa na kujaribu kuwauliza wauguzi ambao pia walibaki kushangaa kuhusu aliko Maduhu ambaye alitakiwa kupelekwa Bugando kwa matibabu ya koo na ambaye hakuna ndugu hata mmoja aliyekuwa anafika kumwona. Mganga mkuu wa hospitali hiyo, Amos Kittoh, alipoulizwa anachojua kuhusu kutoroka kwa mfungwa huyo alijibu: "Nilikuwa likizo, sikuwa najua lakini nafahamu kuwa alitakiwa kwenda Bugando, maana hali yake haikuwa nzuri. Kama ametoroka na kama hatopata matibabu ni maajabu kunusurika kifo... Lakini nitafuatilia,” alisema. Uongozi wa magereza hapa Serengeti haukuwa tayari kuzungumzia suala hilo na juhudi za kumsaka mkuu wa magereza mkoa wa Mara zinaendelea. Kabla ya kujaribu kujiua Novemba 4 baada ya kumuua mkewe na mkwewe, Maduhu alitia kiberiti nyumba yao, kisha akajitundika kwa kamba lakini kamba ilipokatika, ndipo akachukua kisu na kujichinja koromeo. Sababu ya Maduhu kufanya ukatili huo inadaiwa kwamba ni baada ya mkewe kumkataa na kurudi kwao na alipofuatilia ili mama mkwe wake arejeshe sh. 50,000 alizokuwa ametoa kama kishika uchumba, alikataliwa na ndipo akaamua kufanya unyama huo.

Apasua tumbo la mjamzito na kutaka kuiba kichanga

Mwanamke mmoja wa nchini Marekani ( pichani) ambaye alikuwa na ndoto ya kupata mtoto, amefunguliwa mashtaka ya kujaribu kuua baada ya kulipasua kwa kutumia kisu tumbo la mwanamke mjamzito akiwa na nia ya kuiba kichanga kilichokuwa tumboni mwake. Mwanamke mwenye umri wa miaka 40 aliyetambulishwa kwa jina la Veronica Deramous mkazi wa Maryland, Marekani aliwatangazia familia yake pamoja na mpenzi wake kuwa ana mimba na anatarajia mtoto hivi karibuni.Lakini ukweli ni kuwa Veronica hakuwa na mimba na alitiwa mbaroni akikabiliwa na mashtaka ya kujaribu kuua baada ya kulipasua tumbo la mwanamke mjamzito ili amuibie kichanga chake kilichokuwa tumboni.Taarifa ya polisi ilisema kuwa Veronica alitengeneza urafiki na mwanamke mjamzito aliyekuwa hana makazi akilala mitaani akimlaghai kuwa atampa makazi kwenye nyumba yake na atampa vyakula na nguo bure.Lakini mwanamke huyo mwenye umri wa miaka 29 alipoingia nyumbani kwa Veronica, alifungwa mikono yake na kuwekwa mateka kwa siku tano.Taarifa ya polisi iliendelea kusema kuwa Veronica alijaribu kulipasua tumbo la mwanamke huyo ili kukiiba kichanga chake kilichokuwa tumboni.Hata hivyo mwanamke huyo alifanikiwa kutoroka kabla ya Veronica hajakamilisha azma yake baada ya Veronica kupitiwa na usingizi.Mwanamke huyo aliokolewa na polisi waliomkuta kwenye maegesho ya gari ya nyumba hiyo huku akivuja damu kwa wingi.Aliwahishwa hospitali ambako ilibidi azalishwe kwa njia ya upasuaji na mtoto wake wa kike alizaliwa salama akiwa na afya njema na ameamua kumpa jina la "Miujiza".Veronica anashikiliwa na polisi akikabiliwa na mashtaka ya kujaribu kuua na utekaji.

Mzungu awatemea mate Trafiki na Muandishi wa habari na akataa kuhojiwa

AFISA ubalozi wa Canada aliyekamatwa na polisi Kanda maalum ya Dar es salaam kwa tuhuma za kumtemea mate askari wa usalama barabarani mwenye namba E 1653 koplo Samson, amegoma kuhojiwa. Jean Touchatte (48) ambaye ni katibu muhtasi wa ubalozi huo nchini alikamatwa juzi saa 8:15 mchana maeneo ya Banana jijini Dar es Salaam baada ya kumtemea mate askari huyo akiwa kazini. Kaimu Kamanda wa polisi kanda maalum ya Dar es Salaam, Charles Kenyela aliwaambia waandishi wa habari jana kuwa afisa huyo amegoma kutoa maelezo polisi akishinikiza kwanza awepo balozi wake. Alisema siku ya tukio mtuhumiwa huyo ambaye ni katibu muhtasi wa ubalozini hapo, alimtemea mate koplo Samson wakati akiongoza magari yanayotoka Ukonga kuelekea Uwanja wa ndege. Kamanda Kenyela alisema sababu za kumtemea mate askari huyo bado hazijajulikana na mtuhumiwa anashikiliwa kwa uchunguzi zaidi. Alisema baada ya Koplo Samson kutoa taarifa polisi gari hilo lilitangazwa askari waliokuwa doria walioanza kulifuatilia na alipofika barabara ya Nyerere karibu na Kamata gari hilo lilikamatwa na kupelekwa Makao Makuu ya Polisi trafiki Kanda maalum ya Dar es salaam. Kamanda Kenyela alisema wakati mtuhumiwa anaendelea kuhojiwa walifika waandishi wa habari akiwemo Jerry Muro wa TBC kutaka kujua kwa nini katibu huyo alimtemea mate askari. Wakati Jerry anamhoji naye alitemewa mate sehemu ya chini ya kidevu chake na kusambaa katika fulana yake aliyokuwa amevaa kitendo kilichosababisha mwandishi huyo kufungua jalada la shambulio CD/IR/4818/2009. Kamanda Kenyela alisema fulana yenye mate imehifadhiwa kituo cha polisi kati wakati upelelezi unaendelea na kuongeza kuwa maelezo mengine kuhusiana na tukio hilo yatatolewa na Ispekta Jeneral wa Polisi Said Mwema. Awali Kamanda wa kikosi cha Usalama Barabarani, James Kombe, alisema suala hilo walimuachia Mkuu wa Jeshi la Polisi, Said Mwema, ingawa kwa mujibu wa taratibu atafikishwa mahakamani kulingana na uzito wa kosa linalomkabili. Kombe alisema iwapo kosa lake litaonekana kuwa zito ataondolewa ulinzi wake na huenda hatimaye kufukuzwa nchini na kuwahakikishia wananchi kuwa haki itatendeka.

Wednesday, December 9, 2009

Mtuhumiwa wa Mauaji abambwa akiwa amevaa baibui

MWANAFUNZI mmoja wa Shule ya Sekondari anayetuhumiwa kufanya mauaji mkoani Mwanza na kutorokea Shinyanga amekamatwa na akiwa amevaa mavazi ya kike aina ya baibui akiwa katika harakati za kutoroka. Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Shinyanga, Bw. Daudi Siasi amemtaja mwanafunzi aliyekamatwa kuwa ni Daudi Rashidi (18) ambaye pia hutumia jina la Athumani Rashidi anayetuhumiwa kumuua mwanafunzi mwenzake jijini Mwanza wiki iliyopita. Kamanda Siasi alisema mbali ya mwanafunzi huyo ambaye alikamatwa juzi katika kituo kikuu cha mabasi mjini Shinyanga, polisi iliwakamata watu wengine watatuwanaodaiwa kushiriki katika mauaji hayo. Wengine waliokamatwa ni Nixon Robert (18), pia mwanafunzi wa sekondari anayetuhumiwa kushiriki kumpiga mwanafunzi aliyekufa, Bw. Ally Rashid (40) mfanyabiashara wa Mtaa wa Rufiji mjini Mwanza ambaye anadaiwa kuwatorosha wanafunzi hao na Bi. Margaret George (25) mkazi wa Ndembezi, Shinyanga aliyekuwa awapatie hifadhi. Mtuhumiwa Daudi alishtukiwa na abiria wenzake aliokuwa nao katika basi hilo kutokana na sauti yake kuwa ya kiume wakati mavazi aliyokuwa amevaa ni ya kike ikiwa ni baibui nyeusi iliyokuwa imeficha uso wake wote na kuachia uwazi kidogo katika sehemu ya macho na hivyo kutoa taarifa polisi. "Baada ya kuwakamata tuliwasiliana na wenzetu wa Mwanza ambao baada ya kuwatajia majina ya Daud na Nixon waliwatambua kuwa ndiyo wanaowatafuta kuhusiana na kesi yamwanafunzi wa sekondari aliyeuawa kwa kipigo na sasa tunaandaa mipango ili kuwarejesha Mwanza kujibu shtaka la mauaji," alieleza Kamanda Siasi. Hata hivyo, Kamanda huyo alisema kuwa polisi walikuwa na taarifa za siri zilizotolewa na raia wema mkoani Mwanza, kwamba wanafunzi hao na mtu anayewasaidia kuwaficha wametorokea Shinyanga. Kutokana na taarifa hizo na raia walimshtukia mmoja wa watuhumiwa polisi walifanikiwa kuwanasa wakati wakiteremka kwenye basi la Kampuni ya Mohamed Trans mjini Shinyanga.

Uongozi Dar waipiga Stop MAJEMBE kushugulikia Daladala

Uongozi wa Mkoa wa Dar es Salaam, umesimamisha kwa muda shughuli za kampuni ya Majembe Auction Mart za kukamata magari ya daladala ambayo yanakiuka taratibu na sheria za barabarani. Hatua hiyo imechukuliwa baada ya kubainika kuwepo kwa mapungufu mbalimbali ikiwemo ukinzani wa kisheria katika utekelezaji wa agizo hilo, jambo ambalo badala ya zoezi kuwa na manufaa, limegeuka kuwa kero. Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, William Lukuvi, alisema zoezi hilo limesitishwa ili kutoa nafasi kwa wenye magari kujipanga upya kutimiza masharti ya usalama barabarani badala ya kulazimishana. Kampuni ya Majembe ilianza kukamata daladala zinazokiuka sheria wiki iliyopita baada ya kuingia katika mkataba wa mwaka mmoja na Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Majini na Nchi Kavu (Sumatra). Hadi kufikia jana, zaidi ya daladala 400 zilishakamatwa na kutozwa faini kwa makosa mbalimbali, ambapo faini hizo zilikuwa zikilalamikiwa na wamiliki wa daladala kuwa ni kubwa. Faini hizo zilikuwa ni kati ya Sh. 200,000 na 250,000 hatua ambayo iliwafanya madereva kugoma kutoa huduma hiyo juzi katika maeneo ya Tabata, jijini Dar es Salaam.

Akaunti ya EPA kuondolewa BoT?

WAKATI uchunguzi wa Kampuni ya Lazard ya Ufaransa kuhusu hatima ya madai katika Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA) ukiendelea, Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Profesa Benno Ndulu, ametoa msimamo wake akisema BoT haitajihusisha tena na akaunti hiyo iliyokumbwa na ufisadi wa Sh133 bilioni. Tayari BoT kwa kushirikiana na Benki ya Dunia (WB) iliipa kazi ya miezi tisa kampuni hiyo ya Lazard, kuangalia uwezekano wa kuendelea au kutoendelea kulipa madeni ya EPA, kubaini wadai halali na namna ya BoT kuachana na akaunti hiyo.

Bastola yenye risasi yaokotwa ndani ya Daladala Dar

BASTOLA yenye risasi saba imeokotwa ikiwa imetelekezwa na mtu asiyefahamika kwenye daladala jijini Dar es Salaam. Bastola hiyo imeokotwa katika daladala lililokuwa na namba za usajili T 209 AWA linalofanya safari zake kati ya Kariakoo na Tandika. Kwa mujibu wa taarifa hiyo ilisema kuwa bastola hiyo iliyokuwa na risasi saba iliokotwa jana majira ya saa 7 mchana, katika maeneo ya Mtaa wa Msimbazi karibu na kituo kidogo cha Polisi Gerezani.

Tanzania kuazimisha Miaka 48 ya UHURU

LEO tarehe 9 Disemba ni Sikukuuu ya Maadhimisho ya miaka 48 ya Uhuru wa Tanganyika na kitaifa maadhimisho hayo yanaadhimishwa katika viwanja vya Uhuru vya jijini Dar es Salaam. Katika Madhimisho hayo mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Rais wa Jamuhuri wa Muungano wa Tanzania, ambaye pia ni amiri jeshi mkuu, Mh. Jakaya Mrisho Kikwete ambapo atalihutubia taifa katika viwanja hivyo na kukagua gwaride maalumu na vikundi mbalimbali vya halaiki .Pia viongozi mbalimbali wakuu watahudhuria wakiwemo wa Tanzania bara na Tanzania Visiwani.Kauli mbiu ya mwaka huu katika maadhimisho hayo inasema "Tulinde Uhuru na Amani kwa Maendeleo ya Taifa letu".

Mtoto wa Chenge mbaroni kwa kusababisha Ajali

Madina Chenge (25), mkazi wa Oysterbay, jijini Dar es Salaam anayedaiwa kuwa mtoto wa Mbunge wa Bariadi Magharibi, mkoani Shinyanga, Andrew Chenge (CCM), amefikishwa mahakamani kujibu shitaka la kuendesha gari bila kuzingatia sheria za usalama barabarani. Madina alifikishwa jana katika Mahakama ya Wilaya ya Ilala, jijini Dar es Salaam na shitaka lake liko mbele ya Hakimu Samuel Maweda wa mahakama hiyo. Awali hati ya shitaka iliyosomwa mahakamani hapo ikidai kuwa mshitakiwa huyo anadaiwa kutenda kosa Novemba 17, mwaka huu saa 11:30 jioni katika makutano ya barabara ya Umoja wa Mataifa na ya Mt. Imaculata, jijini Dar es Salaam.Ilidaiwa mahakamani hapo kuwa siku ya tukio hilo, mshitakiwa aliendesha vibaya gari lililokuwa na namba za usajili T 193 AYL aina ya Toyota Harrier kwenye barabara hizo na kushindwa kusimama alipofika kwenye barabara ndogo ya Mt. Imaculata.Ilidaiwa kuwa shitakiwa huyo alitakiwa kusimama ili kutoa nafasi kwanza kwa shughuli za kitrafiki katika barabara kuu ya Umoja wa Mataifa kumalizika, lakini matokeo yake mshitakiwa alidaiwa kuendesha gari vibaya bila kufuata taratibu hizo za kitrafiki na kugongana na gari lenye namba za usajili T 958 ATS aina ya Toyota Land Cruiser na kusababisha uharibifu katika magari yote mawili. Hata hivyo, Madina alipewa dhamana ambayo alitakiwa kuwa na wadhamini wawili waliotakiwa kusaini dhamana ya Sh. 500,000 kila mmoja kwa kiwango hicho. Kesi hiyo iliyotajwa kwa mara ya kwanza Novemba 24, mwaka huu, lakini waandishi wa habari hawakuruhusiwa kuiripoti. Kesi hiyo iliahirishwa na itatajwa tena mahakamani hapo kesho. Madina anakabiliwa na kesi hiyo huku baba yake, Andrew Chenge (61), akikabiliwa na kesi ya kuendesha gari kwa uzembe na kusababisha ajali iliyoua wasichana wawili jijini Dar es Salaam, baada ya gari lake kuigonga bajaj Machi, mwaka huu.

Tuesday, December 8, 2009

Didier Drogba kusuuza nyoyo za Watanzania??????

Yule mchezaji mahiri Didier Drogba, Salomon Kalou, Yaya Toure na Kolo Toure, ni miongoni mwa nyota wa kikosi cha timu ya taifa ya Ivory Coast kitakachotua hapa nchini Januari 2 kwa ajili ya kuweka kambi ya wiki moja kwa ajili ya maandalizi ya safari yao ya kwenda nchini Angola kushiriki kwenye Fainali za Mataifa ya Afrika. Ivory Coast chini ya nahodha wao mshambuliaji wa vinara wa Ligi Kuu ya England Chelsea, Drogba, watacheza mechi mbili za kirafiki hapa na timu ya taifa ya Tanzania 'Taifa Stars' kabla ya kuelekea Angola.

Apigwa hadi kupoteza Fahamu kisa kumpiku MUMEWE kwenye Uchaguzi

MWANAMKE Salma Musa mkazi wa Kiloleni Mkoani Tabora, amelazwa katika hospitali ya Mkoa huo baada ya kupigwa na mumewe hadi kupoteza fahamu kwa kile kinachosemekena kushinda uchaguzi wa Mwenyekiti wa Serikali za Mtaa kwa tiketi ya CCM. Mwanamke huyo alipigwa baada ya kumpiku mumewe huyo katika uchaguzi uliofanyika hivi karibuni nchini kote ambapo yeye aligombania kiti hicho kwa tiketi ya CCM na mumewe huyo kugombania kiti hicho kwa tiketi ya CUF.Akielezea mkasa huo kwa waandishi wa habari kwa shida, huku akiwa kitandani katika hospitali hiyo, baada ya kupata fahamu kidogo Salma alisema kuwa sababu iliyomfanya apigwe na mume wake huyo kukerwa na kitendo cha yeye kushinda uchaguzi huo kwa tiketi ya CCM.Alieleza kuwa mume wake huyo alikuwa akimkorofisha kwa muda mrefu na kukerwa na kitendo cha yeye kumpiku katika uchaguzi huo na kusema kuwa yeye alitoa rushwa kwa wasimamizi wa uchaguzi na maneno mengi kuashiria hakushinda kwa halali kwenye uchaguzi huo lazima atakuwa ametoa rushwa ya ngono kwa wasimamizi.Alisema mara kwa mara alikuwa akimpiga lakini alimsihi kuwa aachane na tabia hiyo lakini aliendela na vitendo vya kumpiga mara kwa mara na mara ya mwisho alimwamia kuwa akimpiga anakimbilia polisi kutoa taarifa.Alisema baada ya kumwambia hiyo ndipo alimpiga hadi kupelekea kupoteza fahamu na majirani kukimblia polisi kutoa taarifa kufuatia tukio hilo.Mkuuu wa Wilaya ya Tabora Mussa Chang’a amesema kuwa mume wa dada huyo anashikiliwa na jeshi la polisi kufuatia ukatili huo alioufanya kwa mke wake huyo.

Chanzo cha Ajali SUKA KIMARA chajulikana!!!!!

DEREVA aliyesababisha ajali jana katika eneo la Kimara Suka na kusababisha vifo vya watu wawili papohapo chanzo kilichomfanya asababishe ajali hiyo yahisiwa. Hayo yalijulikana baada ya mwanamke mmoja aliyekuwa akilia kwa uchungu na kupiga kelele zisizo na mfano eneo la tukio huku akinukuliwa maneno na mashuhuda eneo la tukio.Mwanamke huyo ambaye hakutaka kutaja jina lake alisema kuwa hajui atafikaje kwao mkoani Mbeya baada ya mpenzi wake huyo kukamatwa na kupelekwa polisi.Alidai kuwa yeye na dereva huyo walikuwa wakielekea mkoani Mbeya ambapo dereva huyo alikuwa ni mwajiriwa wa kampuni ya Total.Alisema hajui ilikuwaje hadi kutokea ajali hiyo baada ya kulopoka kuwa usiku wa kuamkia safari hiyo walikesha kwenye hoteli moja jijini kwa ajili ya matanuzi na walichelewa sana kulala na asubuhi yake ndipo walipoanza safari hiyo.“ Sijui ilikuwa ni usingizi jamani sijui pombe zilikuwa hazijamtoka au …. Jamani ameshaua nitafanyaje mimi jamani nitafikaje Mbeya mimi? Alijiuliza huku akinukuliwa na baadhi ya watu eneo la tukio bila kujijuaHivyo baada ya kutoa siri hiyo baadhi ya watu kama unavyojua baadhi walianza kumshambulia kwa maneno na kumshutumu kuwa yeye ndiye aliyesababisha ajali hiyo.

HULK HOGAN Kuoa tena?

Kuna habari za kuaminika kuwa mwanamieleka mstaafu HULK HOGAN anataka kuoa tena baada ya kukamilisha talaka na mkewe Linda aliyezaa nae watoto wawili. Inasemekana Hulk anatarajia kumuoa mpenzi wake anayejulikana kama Jennifer McDaniel, kwa sasa Hulk anaonekana kila sehemu akifuatana na Jennifer ambaye ana tatoo ya jina halisi la Hulk "Terry" katika bega lake la kulia.

Mwanamke mwenye umbile dogo duniani ajifungua mtoto wa 3



Stacey Herald,Mama mwenye umbile dogo kuliko wote duniani amejifungua salama mtoto wa tatu pamoja na kwamba madaktari walimuonya kuwa angeweza kupoteza maisha yake kutokana na ukubwa wa tumbo lake ambalo lilimfanya ashindwe kutembea. Mama mwenye umbile dogo kuliko wote duniani ambaye ana urefu wa sentimeta 71 tu, amejifungua salama mtoto wa tatu wa kiume pamoja na kwamba kulikuwa na hofu ujauzito wake ungeweza kusababisha apoteze maisha.Stacey Herald, mkazi wa Kentucky nchini Marekani amejifungua mtoto wa kiume mwenye uzito wa kilo 1.2 ambaye amempa jina la Malachi.Stacey mwenye umri wa miaka 35, ana watoto wawili wa kike aliozaa na mumewe Will mwenye umri wa miaka 27.Stacey alipingana na ushauri wa madaktari kwa mara ya tatu ndani ya miaka mitatu kwa kuzaa watoto watatu ingawa madaktari walimuonya kuwa ujauzito ni hatari kwa afya yake.Mtoto wake watatu alizaliwa wiki iliyopita kabla ya muda wake akiwa na wiki 32 tu tumboni baada ya madaktari kuona kuwa kwa jinsi tumbo la Stacey lilivyozidi kuwa kubwa, viungo vyake vya ndani vingeweza kupasuka.Stacey ameruhusiwa kurudi nyumbani kwake ingawa mtoto wake ataendelea kubakia hospitali akipatiwa matibabu zaidi.Stacey anasumbuliwa na ugonjwa unaoitwa Osteogenesis Imperfecta, ambao husababisha mifupa kuwa dhaifu yenye kuvunjika kirahisi, mapafu dhoofu na ugonjwa huo umemsababishia asirefuke.Mumewe ana urefu wa mita 1.71 na watoto wao wawili hivi sasa wameisharefuka kuzidi urefu wa mama yao.Mtoto wake wa kwanza Kateri alizaliwa mwaka 2006 akiwa na urefu nusu ya urefu wa mama yake kwa bahati mbaya alirithi ugonjwa wa mama yake kwahiyo naye pia hatarefuka atakuwa kama mama yake.

Monday, December 7, 2009

Mambo usiyoyajua kuhusu Ernest Semayoga - Mfungwa aliyepata Digrii ya Sheria akiwa kifungoni

Semayoga (37) ambaye ni kijana mtanashati aliyezaliwa mwaka 1972, alitunukiwa shahada hiyo na Mkuu wa Chuo Kikuu Huria Tanzania (OUT), Dk. John Malecela katika hafla ya pekee iliyohudhuriwa na viongozi mbalimbali akiwemo Makamu Mkuu wa Chuo hicho, Tolly Mbwete, Waziri wa Mambo ya Ndani Lawrence Masha, Mkuu wa Magereza, Kamishna Augustino Nanyaro na wafanyakazi mbalimbali wa OUT na Magereza. Sherehe hiyo iliyopambwa na bendi ya Polisi pia ilihudhuriwa na ndugu wa Semayoga, waandishi wa habari pamoja na wanajeshi waliokuwa wakitumbuiza katika hafla hiyo kwa bendi yao. Semayoga, ni mmoja wa wahitimu wa mwaka huu wa Chuo Kikuu Huria (OUT) katika sehemu ya pili ya Mahafali ya 21 ya chuo hicho yaliyofanyika katika viwanja vya Kikosi Maalumu cha Kuzuia Ghasia Magerezani, Ukonga, Ilala, jijini Dar es Salaam. Mahafali hayo yalifanyika katika nyakati mbili tofauti ambapo mfungwa huyo alifanyiwa ya kwake Desemba mosi tofauti na wahitimu wenzake waliofanyiwa ya kwao Novemba mwaka huu kutokana na masharti ya Sheria za Magereza. Kijana huyo mwenye mke na mtoto mmoja anayeitwa Astrida Michael anayesoma kidato cha sita katika Shule ya Sekondari ya St. Mary iliyoko Mbezi jijini Dar es Salaam alipopata wasaa wa kuzungumza, baada ya kupata shahada yake kwa kujiamini aliiomba serikali iwasamehe wafungwa waliojirekebisha. Mfungwa huyo anayetarajia kumaliza kifungo chake Agosti mwakani, anasema mfungwa aliyeonesha kujifunza na kujirekebisha anaposamehewa, husaidia kuwashawishi wafungwa wengine kubadili tabia na kujiandaa kwa ajili ya maisha yao baada ya kutoka gerezani. Semayoga ambaye ana ndoto za kujiunga na Shahada ya Uzamili ya Sheria (LLM), anaelezea historia yake kuwa alizaliwa mkoani Kigoma na kusoma Shule ya Msingi ya Kigoma mnamo mwaka 1981 hadi 1987 na alipomaliza darasa la saba, alichaguliwa kujiunga na Shule ya Sekondari ya Kilosa alikosoma kidato cha kwanza na pili. Alipofika kidato cha tatu alihamia Shule ya Sekondari Kigoma alikomaliza kidato cha nne mwaka 1991 na kufanikiwa kujiunga na kidato cha tano na sita katika Shule ya Sekondari ya Azania alikokuwa akichukua masomo ya Fizikia, Kemia na Biolojia (PCB). Alimaliza kidato cha sita mwaka 1994 lakini hakufanikiwa kuendelea na elimu ya juu kwa kuwa alifiwa na mama yake mzazi msiba ambao anasema ulisababisha achanganyikiwe na kushindwa kuendelea na shule. “Baada ya muda nilianza kufanya biashara mbalimbali na baadaye nilishawishika kufanya biashara haramu ya kuuza dawa ya kulevya toka nchini Mauritius kwenda Afrika Kusini na Tanzania,” anasema. Mwaka 1999 akiwa njiani kutoka nchini Afrika Kusini kuja Tanzania kupitia Mauritania akiwa na dawa za kulevya, alikamatwa na kufungwa nchini humo hadi mwaka 2006 aliporejeshwa nchini Tanzania kuendelea na kifungo chake. Anasema alifikia katika Gereza la Ukonga na mwaka 2007 ambapo aliamua kujiunga rasmi na OUT kuchukua masomo ya sheria ili kusaidia wafungwa kwa kuwa hawafahamu haki na taratibu zao na kuongeza kuwa amekuwa akiwasaidia kuandaa rufaa zao. Anasema kaka yake mkubwa Dk. Francis Semayoga, ambaye ni Mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) ndiye aliyemhamasisha kuanza masomo katika chuo hicho na kwa kushirikiana na OUT walimpatia vitabu na vifaa mbalimbali vya kusoma. Akizungumzia changamoto anazopata anasema kubwa aliyokabiliana nayo ni pamoja na kutokuwa na muda maalumu wa kusoma kwa kuwa ni lazima kufuata taratibu za gerezani ambapo anapaswa kulala saa tisa mchana, ingawa kwa sasa magerezani hali imebadilika siyo kama ilivyokuwa hapo zamani, lakini dhana ya kurekebisha watu tabia inatakiwa kuboreshwa ili anapotoka gerezani, awe mtu mpya. Anasema serikali inapaswa kuboresha mazingira ya kusoma kwa ajili ya wafungwa kwa sababu wapo wengi wanotamani kusoma lakini hawajafikia kiwango cha elimu kinachohitajika wakubalike kujiunga na elimu ya juu. Dada mkubwa wa Semayoga, Theobaldina Kasakanta anasema Semayoga ambaye ni mdogo wao wa sita na ni kati ya kaka zao wanne na dada watatu ambapo mmoja alifariki mwaka jana. Anasema wanamshukuru Mungu kwa hatua aliyoifikia mdogo wao kwa kuwa wamepata faraja kwani baada ya kufungwa waliona wamempoteza lakini kwa sasa baada ya kupata shahada, wanaamini akimaliza kifungo atakuwa mtu mpya katika familia. Anasema tangu utoto wake Semayoga hakuwa na makuu na kwamba siku zote alikuwa na upendo. Anasema kasoro iliyojitokeza ya kujiingiza katika biashara ya dawa za kulevya ilisababishwa na kudanganyika tu akiwa katika jitihada za kutafuta maisha. Hata hivyo dada huyo anasema yeye na ndugu wengine wamefanikiwa kuhudhuria mahafali hayo lakini mkewe Semayoga yuko masomoni nchini Marekani na mtoto wake yuko katika ziara ya kimasomo mkoani Morogoro na hivyo hawakuhudhuria. Rafiki wa Semayoga aliyetoka katika mji wa Kahama mkoani Shinyanga kushuhudia mahafali hayo ambaye pia anaitwa Ernest waliyesoma naye Shule ya Sekondari ya Kilosa, anasema rafiki yake huyo alikuwa na akili sana katika masomo huku akipenda kila mwanafunzi aelewe. Anasema mara kwa mara nyakati za jioni wanafunzi wenzake walimfuata kuomba awafundishe kile walichokuwa hawajaelewa. Anasema anahisi kitendo cha rafikiye kujiingiza kuuza dawa za kulevya kilikuwa cha bahati mbaya akiwa katika kutafuta maisha.

Ajali Mbaya yatokea KIMARA SUKA Wawili wafa mmoja ajeruhiwa

Tukio hilo la kusikitisha limetokea asubuhi hii, majira ya saa mbili, katika eneo la Kimara Suka, baada ya mafundi 3 kukanyagwa na matairi baada ya lori lingine kusukumiza lori ambalo walikuwa wakitengeneza wao.Mafundi hao walikuwa wakitengeneza gari aina ya lori lililokuwa na namba za usajili T.427 AGX aina ya Scania ambalo liliharibika tokea juzi usiku eneo hilo ambalo walikuwa wakielekea mjini Arusha.Juhudi za mafundi hao jana kutwa nzima ziligonga mwamba baada ya kushindikana kuondoa lori hilo ambapo juhudi za mafundi hao zilitarajiwa kuzaa matunda asubuhi hii kwa kuwa katika hatua za mwisho katika kuondoa gari hilo ambalo liliharibika eneo hilo.Ilidaiwa kuwa mafundi hao watatu asubuhi hii walikuwa katika hatua za mwisho ambapo walishafanikiwa kukamilisha kitu ambacho kilikuwa kinakorofisha kwa siku mbili hizo.Hivyo bila kutarajia mafundi hao wkati wapo chini ya uvungu wa gari kukamilisha gari hilo kwa ajili ya kuanza safari, papohapo lilitokea lori jingine nyuma na kugonga lori hilo kwa nyuma na kuwasaga mafundi hao ambao walikuwa wakitengeneza lori hilo.Lori hilo lilisukumizwa kwa mbele na kufanya mafundi hao mmoja kusagwa kichwa na mwingine akiwa katika juhudi za kijitetea alichelewa na kusagwa na tairi maeneo yake ya kiuno.Mmoja kati ya mafundi hao alikuwa upande mwingine na alibahatika kuruka na kuacha mafundi wenzake wawili kufariki papohapo.Ilidaiwa kuwa baada ya kusababisha ajali hiyo dereva wa lori ambalo lilisababisha ajali ambaye hakuonyesha ushirikiano kwa kukataa kutaja jina lake alikuwa anajaribu kutaka kukimbia na wananchi wakamuwahi na kubaki hapo ambalo lori hilo lilikuwa na namba T 282 ADH aina ya Scania.

VJN Super Motors

Wauzaji Mahiri wa Spare za Pikipiki na Magari yote toka Europe na Japan, Tupo Mtaa wa Msikitini Musoma Mjini, Pia tunaweza kutoa hudumu kwa watu wa Dar es salaam, Wasiliana nasi kwa Sanduku la Barua 557 Musoma, Simu No. 0282620610 , Barua pepe : vincent_nye@yahoo.co.uk. Karibuni wote