Uwepo wa Site hii Unategemea sana Ushirikiano wangu na wako, na ni njia mojawapo ya kuonyesha mshikamano na Jamii inayotuzunguka , PLS Usisite kunitumia Habari au kitu chochote chenye Uhakika ambacho hisia zako zitakupeleka kuwa kitaleta Mabadiliko na mafunzo katika jamii, Kumbuka kuwa msaada si Fedha wala Lulu bali chochote kinachoweza kuleta mabadiliko katika Maisha ya mtu mwingine. Kwa lolote usisite kuwasiliana nami kupitia chingasite@gmail.com au tumainijhn@yahoo.co.uk au simu No. 0712221744 na 0787221744. Karibuni Wote
Powered By Blogger

Wednesday, October 28, 2009

Mwakyembe agoma kuhojiwa na Takukuru

Mbunge wa Kyela (CCM), Dk. Harrison Mwakyembe, amegoma kuhojiwa na Taasisi ya Kuzuia na Kudhibiti Rushwa (Takukuru) kwa madai kuwa, hatua hiyo ina lengo la kuwatisha na kuwafumba midomo wabunge. Pia, Dk Mwakyembe amesema Takukuru haikupaswa kuwahoji wabunge katika kipindi hiki ambacho Bunge linasubiri taarifa ya serikali kuhusu utekelezaji wa maazimio 23 ya Richmond, likiwemo kumchukulia Mkurugenzi Mkuu wake, Dk. Edward Hoseah, ambaye anadaiwa kuisafisha kampuni hiyo ya kitapeli. Dk. Mwakyembe alisema hayo wakati akizungumza na waandishi wa habari mjini hapa jana kuhusu taarifa zilizochapishwa na gazeti moja la kila siku (si Nipashe), likielezea kuhusu kuhojiwa kwake na Takukuru. “Takukuru walinipigia simu niende kuhojiwa nikakataa kwa sababu mazingira yaliyopo yanaonyesha wanataka kuwanyamazisha wabunge, hiyo ni kinyume cha Sheria ya Kinga, Madaraka na Haki za Bunge,” alisema Dk. Mwakyembe, ambaye alikuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Teule ya Bunge kuchunguza mchakato wa utoaji wa zabuni ya kuzalisha umeme wa dharura wa megawati 100 kwa kampuni ya Richmond. Dk. Mwakyembe ambaye pia ni mwanasheria aliyebobea, alisema kitendo cha kukataa kuhojiwa na Takukuru hakipaswi kutafsiriwa kwamba ni kuhamaki kama ilivyoripotiwa na gazeti hilo, bali ni ujasiri unakidhi matakwa ya kisheria, kanuni na taratibu.
“Bunge linapokuwa kwenye mchakato wa kutaka Mkurugenzi Mkuu wa Takukuru achukuliwe hatua, kisha taasisi hiyo ikaanza kuwahoji wabunge wanaosubiri utekelezaji wa maagizo waliyoyatoa, ni kinyume cha utawala wa sheria,” alisema. Kwa mujibu wa Mwakyembe, watendaji wa Takukuru walianza kuwahoji wabunge mbalimbali katika kipindi cha zaidi ya mwezi mmoja, wakitaka taarifa kuhusu madai ya wabunge kupewa posho wanapotembelea taasisi za umma, licha ya kulipwa stahiki zao na ofisi ya Bunge. Dk. Mwakyembe alisema hatua iliyochukuliwa na Takukuru kuwahoji wabunge, inatia mashaka hasa kwa vile taasisi hiyo imewahi kuwalipa posho wabunge mara kadhaa. Kwa upande mwingine, Dk. Mwakyembe alisema watuhumiwa wa ufisadi wanatumia baadhi ya vyombo vya habari (akivitaja jina) kuwachafulia majina wananchi wanaotetea maslahi mapana ya umma. “Si jambo la ajabu nilivyoandikwa na gazeti la (analitaja jina), hili linamilikiwa na mafisadi, linatetea maslahi ya mafisadi kiasi cha kupoteza mvuto wake kwa wasomaji,” alisema mbunge huyo machachari.
Suala la kuhojiwa kwa wabunge kuhusiana na posho wanazodaiwa kuchua mara mbili, kwenye Bunge na kwa taasisi wanakofanya kazi, linaelezwa kuwa ni juhudi za kutaka kupunguza makali ya wabunge. Jana baadhi ya wabunge waliozungumza na gazeti hili kwa masharti ya kutotajwa majina yao, walisema wanaona mbinu hizi kama mapambano ya kitaasisi. Takukuru mwishoni mwa wiki walitoa taarifa kwa vyombo vya habari wakisema wabunge kama walivyo wananchi wengine wanawajibika kuitikia mwito wao wa kuhojiwa katika masuala mbalimbali yanaohusiana na rushwa.

No comments:

VJN Super Motors

Wauzaji Mahiri wa Spare za Pikipiki na Magari yote toka Europe na Japan, Tupo Mtaa wa Msikitini Musoma Mjini, Pia tunaweza kutoa hudumu kwa watu wa Dar es salaam, Wasiliana nasi kwa Sanduku la Barua 557 Musoma, Simu No. 0282620610 , Barua pepe : vincent_nye@yahoo.co.uk. Karibuni wote