Mwanasiasa mkongwe Zanzibar, Ali Ameir Mohammed, ametangaza kung’atuka kuwania ubunge katika uchaguzi mkuu ujao. Ali Ameir ambaye kwa sasa ni Mbunge wa Donge, Kaskazini Unguja, amewahi kushika nyadhifa mbalimbali katika Serikali ya Muungano pamoja na Chama cha Mapinduzi (CCM). Amesema ameamua kutogombea tena ubunge ili apumzike. Alisema uamuzi huo ni wake binafsi na kwamba hakuna kituo chochote kilichotaka aendelee kuwa mbunge wao.Alisema wananchi wa Donge bado wana imani na utumishi wake na hata kama wangejitokeza wanachama 100 kupambana naye angeweza kushinda. Alisema tayari wazee wa Donge wamekubali uamuzi wake wa kutogombea ingawa kwa kinyongo. Hata hivyo alisema uamuzi wake wa kustaafu huuna nia ya kuwashawishi wazee wengine kufuata nyayo zake kwa kuwa suala hilo ni hiari ya mtu. Miongoni mwa nyadhifa alizowahi kushikilia Mbunge wa jimbo hilo ni Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Mshauri wa Rais wa Zanzibar wa masuala ya siasa, Waziri wa Habari na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi. Ameir ni mwanasiasa wa pili mkongwe kutangaza uamuzi kama huo Zanzibar. Mwingine ni Mbunge wa Makunduchi, Abdusalami Isaa Khatib, ambaye ameshasema kuwa hatagombea mwaka huu. Khatib hivi sasa ni Mbunge wa Makunduchi, Mkoa wa Kusini Unguja.
Chanzo: Nipashe
No comments:
Post a Comment