MAHAKAMA Kuu Kanda ya Dar es Salaam imepokea waraka ambao inadaiwa uliandikwa na Benson Urio kabla ya kutenda kosa baada ya kushtakiwa kwa jaribio la mauaji. Katika kesi hiyo namba moja ya mwaka 2008, Benson anadaiwa kujaribu kumuua aliyekuwa mpenzi wake, Omega Leweta ambaye ni mkazi wa Kimara jijini Dar es Salaam baada ya kumvizia akiwa usingizini na kuanza kumkatakata kwa mapanga sehemu mbalimbali za mwili. Pia mshtakiwa huyo anadaiwa kuwa baada ya kumkatakata mpenzi wake, Benson pia anadaiwa kujikatakata shingoni kwa panga kwa lengo la kujiua sambamba na mpenzi wake huyo. Waraka huo ambao unadaiwa kuandikwa na mshtakiwa huyo kwenda kwa mama yake mzazi, Felister Urio ulisomwa juzi mahakamani hapo na shahidi wa tano katika kesi hiyo D/Sgt. Gotard Ipande wakati akitoa ushahidi katika kesi hiyo. Waraka huo unaonyesha dhamira ya mshtakiwa huyo kumuua mpenzi wake na baadaye kujiua. Katika waraka huo, Benson anaeleza jinsi mama yake alivyomlea na kumtakia maisha mema, lakini baadaye anaanza kueleza jinsi alivyopendana na mpenzi wake hadi wakati anaondoka kwenda Ulaya. Anaeleza jinsi alivyokatisha maisha yake ya barani Ulaya na jinsi ambavyo mpenzi wake hakufurahia kurejea kwake mapema na baadaye kueleza jinsi mpenzi huyo alivyobadilika baada ya kurejea. "Hali niliyokukuta nayo haikuwa nzuri kama nilivyokuzoea. Nilikuuliza una tatizo gani ukajibu hakuna tatizo. Nilikuuliza au umepata mpenzi mwingine ukasema hakuna. Nilivyokufahamu siyo ulivyokuwa na siku zilivyozidi kwenda nilikuuliza kila tulivyozoeana," anasema katika waraka huo. Hadi leo uhusiano wangu kwake hauko, hata ya kusema anachonisemesha ni salamu tu, habari za asubuhi na za saa hizi atokapo kazini. Hata wakati wa kula ni mende tu ndio wanamfukuza chumbani na kumwambia nenda kakae na mwenzako umemwacha; Hata nikimsemesha anaitikia tu sasa jamani naomba kuuliza, ni mapenzi gani haya? Je ni kwa sababu ya kusafiri kwangu? Je, ni kwa sababu ya umaskini wangu jamani kwa vile sina pesa, anahoji. "Uhusiano kwangu si mzuri, isitoshe kashfa na dharau na kejeli zimezidi;Nimegundua Omega ana kiburi kwa sababu ana pesa, siku hizi anajuana na watu wengi, lakini kazi anayofanya katafutiwa na dada yangu Happy lakini leo hata Happy hamthamini." Anaendelea kueleza katika waraka huo kuwa anahisi mpenzi wake alipata bwana wakati akiwa Ulaya na anamshangaa kwa jinsi asivyojielewa kwa kuwa alikuwa mpishi wa chakula, maarufu kama "Mama Ntilie". Anaeleza jinsi alivyomsomesha mwanae Grace tangu darasa la nne hadi sekondari. Anaeleza jinsi alivyotuma dola za Kimarekani 250 na baadaye Sh5.5 milioni kwa ajili ya ubarikio wa Grace na zawadi nyingi zenye thamani ya dola 300 za Kimarekani wakati aliporejea nchini, lakini bado anadharaulika na anamaliza waraka wake kwa kueleza kuwa hana deni bali yeye ndiye anayewadai watu aliowataja na kwamba vitu vyote apewe mama yake.
Chanzo Mwananchi
No comments:
Post a Comment