Upande wa Jamhuri katika kesi ya matumizi mabaya ya ofisi na kuisababishia serikali hasara ya Sh. bilioni 221.1 dhidi ya aliyekuwa Mkurugenzi wa Utumishi na Utawala wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Amatus Liyumba, umeiomba mahakama kumuona ana kesi ya kujibu. Upande wa Jamhuri umetoa hoja hiyo kwa kubainisha kuwa Liyumba alihusika kupitisha malipo ya ujenzi wa ghorofa kabla ya kibali cha bodi ya BoT. Wakijibu hoja za upande wa utetezi, upande wa Jamhuri umedai kuwa Liyumba anadaiwa kufanya mabadiliko hayo katika mradi huo bila kwanza kuomba idhini ya bodi na badala yake aliomba kibali baada ya kufanya mabadiliko. Hoja hizo zimewasilishwa jana alasiri katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam. Ilidaiwa kuwa katika ushahidi uliotolewa na mashahidi nane dhidi ya mshitakiwa huyo, ni rai ya upande wa Jamhuri kwamba mahakama imuone mshitakiwa ana kesi ya kujibu. Hata hivyo, mahakama baada ya kupokea hoja za pande zote mbili kwa njia ya maandishi, hatma ya Liyumba kujitetea au kuachiwa huru itajulikana Aprili 9, mwaka huu. Pia upande huo wa mashtaka umeeleza kwamba ushahidi huo na kupitia vielelezo 13 vinatosha kabisa kuishawishi mahakama kumuona mshtakiwa ana kesi ya kujibu. Machi 22, mwaka huu, upande wa utetezi uliomba mahakama kumuona mshitakiwa hana kesi ya kujibu baada ya ushahidi uliotolewa kutokuwa na nguvu hivyo mahakama imuachie huru. Machi 15, mwaka huu upande wa mashtaka ulifunga ushahidi dhidi ya kesi hiyo ambapo mahakama iliamuru pande zote ziwasilishe hoja za kama mshtaka ana kesi ya kujibu au la, kwa njia ya maandishi.
Chanzo: Nipashe
No comments:
Post a Comment